Home » » SERIKALI YATILIA UMUHIMU KUCHIMBA GRAPHITE

SERIKALI YATILIA UMUHIMU KUCHIMBA GRAPHITE

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399.
Waziri wa Nishati na Madini, Profesa Sospeter Muhongo.
WAZIRI wa Nishati na Madini, Profesa Sospeter Muhongo ameeleza kuwa Serikali inatoa kipaumbele katika uchimbaji wa madini ya graphite nchini kutokana na umuhimu wake duniani ikiwemo kutumika kama malighafi ya kutengenezea betri za simu, kalamu za risasi na kompyuta mpakato.

Aliyasema hayo wakati alipokutana na Kampuni ya Tanzgraphite (TZ) ambayo ni kampuni tanzu ya Kibaran Resources inayofanya utafiti wa madini hayo tangu mwaka 2012 eneo la Epanko wilaya ya Ulanga, Morogoro.

Kwa mujibu wa taarifa ya wizara hiyo, Profesa Muhongo alisema madini hayo yana soko kubwa duniani kwani hutumika pia katika utengenezaji wa vilainishi mbalimbali. Profesa Muhongo alitoa kauli hiyo baada ya Mkurugenzi Mtendaji wa kampuni hiyo, Jacka Mwambi kumueleza kuwa kampuni hiyo imepanga kuanza uzalishaji wa madini hayo mwaka 2017 lakini ili kutekeleza hilo kwa ufanisi, wanahitaji msaada serikalini ikiwemo wa ujenzi wa kituo cha kupoozea umeme cha Ifakara kitakachowasaidia kupata umeme wa uhakika katika eneo la uzalishaji.

Mwambi alisema pia wanaiomba serikali kukamilisha ujenzi wa daraja litakalokatisha mto Kilombero ambalo litawapa uhakika wa usafirishaji wa madini hayo tofauti na kivuko kinachotumika sasa.
“Changamoto nyingine ni baadhi ya wananchi wanaozunguka eneo hilo la uchimbaji ambao wanaonekana kutokukubaliana na mradi kufanyika katika eneo husika, tumejaribu kujadiliana nao kwa kuhusisha ngazi mbalimbali za uongozi lakini bado kuna changamoto ya mawasiliano chanya kati ya kampuni na wananchi,” alisema Mwambi.

Akizungumzia uchimbaji wa madini ya graphite duniani, Mwambi alisema kwa sasa nchi za China, Brazil na India ndizo zinaongoza kwa usambazaji wa madini hayo ambazo wanazalisha tani milioni 1.2 kwa mwaka.
Alisema kwa Afrika, Msumbiji imeonekana kuwa na mashapo mengi na kueleza kuwa endapo Tanzania itafanikiwa kuchimba madini hayo katika eneo la Epanko, itaifanya kuwa mzalishaji mkubwa wa madini hayo barani Afrika.

Alisema gharama ya uendeshaji wa mradi huo wa Epanko itakuwa ni Dola za Marekani milioni 77.5 na uhai wa mgodi unatarajiwa kuwa miaka 25. Alisema faida zitakazotokana na uzalishaji wa madini hayo wilayani Ulanga ni pamoja na ajira 1,500 za moja kwa moja huku akieleza kuwa ajira zisizo za moja kwa moja zitaongezeka mara sita zaidi ya zile za moja kwa moja, pia wafanyakazi katika kampuni hiyo wenye ujuzi na wasio na ujuzi watapatiwa mafunzo ya kuwaendeleza.

Kuhusu changamoto ya wananchi kuchelewesha utekelezaji wa mradi huo, Profesa Muhongo ametuma timu ya wataalamu kutoka Wizara ya Nishati na Madini kwenda katika eneo hilo kuzifahamu changamoto hizo kwa undani na kuwasilisha kwake ripoti keshokutwa saa nne asubuhi.
CHANZO: HABARI LEO

0 comments:

 
Supported by : Tone Media
Copyright © 2012. Morogoro Yetu - All Rights Reserved
Template Modify by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa