Home » » BAJJETI YA DAWA, VITENDANISHI KUFIKIA BILIONI 350/-

BAJJETI YA DAWA, VITENDANISHI KUFIKIA BILIONI 350/-

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399.
Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Ummy Mwalimu akiwa kwenye wadi ya wazazi katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Morogoro
SERIKALI ya Awamu ya Tano imejipanga kutatua changamoto za upatikanaji wa dawa katika hospitali zake nchini kwa kuongeza bajeti ya dawa na vitendanishi kutoka bajeti ya Sh bilioni 70 mwaka uliopita hadi kufikia Sh bilioni 350 kwa mwaka 2016/2017.
Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Wazee na Watoto, Ummy Mwalimu alisema hayo juzi wakati akizungumza na watumishi wa Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Morogoro.
Ummy alisema kuwa lengo la kuongeza bajeti hiyo ni kuhakikisha kuwa huduma za afya katika zahanati, vituo vya afya na hospitali za wilaya zinapatikana kwa uhakika ili kuwapunguzia wananchi changamoto za ukosefu wa dawa na vifaa tiba wakati wanapokwenda kupata huduma.
“Naomba bajeti hiyo ipitishwe na Bunge ili kuwezesha upatikanaji wa dawa kwa uhakika katika hospitali za serikali nchini,” alisema Ummy.
Hivyo alitumia fursa hiyo kuwakumbusha watumishi wa sekta ya afya kujenga mahusiano mazuri na wananchi pindi wanapokwenda kupata huduma ili huduma wanazozitoa ziendane na viapo vya utumishi wao ili kuepuka hali ya sintofahamu iliyoibuka siku za hivi karibuni ambapo madaktari na wauguzi kupigwa na wananchi katika maeneo ya kazi.
Pamoja na hayo, alimwomba Mkuu wa Mkoa wa Morogoro, Dk Kebwe Steven kuwasiliana na Kamanda wa Polisi wa Mkoa kwa lengo la kuwahakikishia usalama wauguzi, madaktari wanaotishiwa maisha na baadhi ya ndugu wa wagonjwa ili pande zote mbili ziwe katika hali ya usalama na kunufaika na huduma za matibabu bila ya vikwazo.
Pia aliwataka watendaji na watumishi katika hospitali na vituo vya afya kuwa wawazi kwa kuweka matangazo kwenye mbao za matangazo juu ya gharama halisi za vipimo au upasuaji ili wananchi wajue gharama halisi.
Kwa upande wake Mganga Mfawidhi wa Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Morogoro Dk Rita Lyamuya, alisema kuwa hospitali hiyo imefanikiwa kuongeza mapato yake katika duka la dawa kutoka mtaji wa Sh milioni tano hadi milioni 120 licha ya kukabiliwa na changamoto mbalimbali za uchakavu wa majengo na miundombinu yake.
Dk Lyamuya alisema kuwa mbali na mafanikio hayo , Hospitali ya mkoa ilishika nafasi ya pili kwa usafi katika hospitali za rufaa hapa nchini na uboreshaji wa huduma za afya kwa wazee kwa kuanzisha dawati maalumu limepewa jukumu la kushauri na kuwahudumia wazee wanapofika hospitalini kupata huduma.
Alisema, pamoja na mafanikio hayo, zipo changamoto mbalimbali hususan ukosefu wa watumishi 75, akiwemo daktari bingwa wa macho, uchakavu wa chumba cha kuhifadhi maiti, majokovu, uzio wa hospitali na ufinyu wa bajeti ya uendeshaji na kutokuwepo kwa mtaalamu wa Tehama.
CHANZO: HABARI LEO.

0 comments:

 
Supported by : Tone Media
Copyright © 2012. Morogoro Yetu - All Rights Reserved
Template Modify by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa