Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399.
UONGOZI wa Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo (SUA) mkoani Morogoro
umesema hakuna mgomo baridi uliofanywa na wahadhiri wa chuo hicho, bali
ni vikao vya baraza la wanataaluma.
Hayo yalisemwa na Makamu wa Mkuu wa chuo hicho, Profesa Gerald Monela
juzi ofisini kwake wakati akizungumza na waandishi wa habari na kutoa
ufafanuzi juu ya kujitokeza kwa uvumi ndani na nje ya Chuo Kikuu hicho
kuwa wanataaluma waliingia kwenye mgomo baridi.
Makamu wa Mkuu wa chuo hicho, alisema Baraza la Wanataaluma (SUASA)
halikuitisha mgomo baridi isipokuwa lilikuwa na vikao vya kawaida
vilivyochukua muda wa siku tatu kwa siku tofauti.
Alisema hali hiyo ilivyotafsiriwa na baadhi ya wanafunzi na watu
wengine wakiwemo wanajamii katika chuo hicho kuwa wahadhiri wa SUA wapo
katika mgomo ama mgomo baridi.
Alisema ulilazimika kuendelea kwa siku mbili zaidi kutokana na unyeti
wa masuala waliyokuwa wakijadiliana na mengine yakitakiwa kutolewa
ufafanuzi wa kina na Menejimenti ya chuo hicho.
Kwa mujibu wa Profesa Monela, mkutano huo wa wanataaluma ulikuwa ni wa 67 na hufanyika kila mwaka kwa siku moja.
Hivyo alisema kikao cha baraza hilo kilikutana Januari 28 na 29 na
kuendelea kufanyika tena Februari mosi mwaka huu kuanzia asubuhi hadi
mchana, lilikuwa linajadili masuala mbalimbali yanayowahusu wanataaluma
hao.
“Chama cha Wanataaluma wa SUA kiliitisha mkutano wao uliofanyika
Alhamisi ya Januari 28, mwaka huu kuanzia saa 8:00 mchana na kawaida
unakuwa ni wa siku moja tu,” alisema Profesa Monela na kuongeza: “Lakini
kutokana na unyeti wa masuala waliyokuwa wakijadili walihitaji kupata
ufafanuzi wa menejimenti na niliitwa kwenye kikao hicho.”
CHANZO : HABARI LEO.
0 comments:
Post a Comment