Home » » MOCHWARI MORO KUKARABATIWA.

MOCHWARI MORO KUKARABATIWA.

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399.
SERIKALI ya Mkoa wa Morogoro imeanza kuchukua hatua mbalimbali za kuboresha mazingira ya kuhifadhia maiti katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa huo ili kuwezesha kukidhi mahitaji ya sasa.
Hatua hiyo imeanza kuchukuliwa kwa kushirikiana na hospitali hiyo kutafuta wadau wa kusaidia kufanya ukarabati mkubwa wa jengo la kuhifadhi maiti ikiwa ni kuweka majokofu mapya.
Mganga Mfawidhi wa Hospitali ya Rufaa ya Mkoa huo, Dk Rita Lyamuya alisema hayo jana mjini Morogoro wakati akizungumza na waandishi wa habari kuhusu utendaji kazi zinazofanyika hospitalini hapo.
Shughuli hizo ni za utoaji wa huduma za tiba kwa wagonjwa wa nje na wanaolazwa na namna ya mazingira ya kuhifadhi maiti za watu wanaokufa kwa ajali, vifo vya kawaida ama maiti zinazookotwa na kuletwa na Polisi hospitalini kwa ajili ya kuhifadhiwa.
Dk Lyamuya alisema Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Morogoro ndiyo pekee inayotegemewa na Halmashauri ya Manispaa ya Morogoro na Halmashauri ya Wilaya ya Morogoro kutokana na kutokuwepo kwa hospitali za wilaya.
Alisema kushamiri kwa matukio ya ajali za barabarani, majeruhi na watu wanaopoteza maisha, miili yao inaletwa hospitali ya rufaa ya mkoa na kuhifadhiwa chumba za maiti kilichopo katika hospitali ya rufaa ya mkoa.
Alisema chumba cha kuhifadhi maiti katika hospitali ya rufaa hiyo kina majokofu manne yenye uwezo wa kuhifadhi maiti 30, lakini hadi sasa ni jokofu moja lenye uwezo wa kuhifadhi maiti sita ndilo linalifanya kazi.
Pamoja na hayo, alisema majokofu mengine mawili katika chumba hicho ambalo kila moja lina uwezo wa kuhifadhi maiti sita yanafanyiwa matengenezo kutokana na hitilafu iliyokuwa imejitokeza.
“Kukamilika kwa matengenezo ya majokofu haya kutawezesha hospitali ya rufaa ya mkoa ambayo ndiyo tegemeo kubwa kuwa na uwezo wa kuhifadhi maiti 18,” alisema Dk Lyamuya na kuongeza kuwa jokofu moja lenye uwezo wa kuhifadhi maiti 12 halifanyi kazi kutokana na ubovu, hivyo kuhitajika kununuliwa jingine ama kufanyiwa matengenezo makubwa sambamba na maboresho ya mfumo mzima ya jengo hilo.
CHANZO : HABARI LEO.

0 comments:

 
Supported by : Tone Media
Copyright © 2012. Morogoro Yetu - All Rights Reserved
Template Modify by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa