Home » » VIWANDA MORO VYAPIGWA FAINI.

VIWANDA MORO VYAPIGWA FAINI.

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399.
Naibu Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira), Luhaga Mpina.
Rungu la faini kutokana na ukiukwaji wa sheria za mazingira limeendelea kuviandama viwanda mbalimbali vya mkoa wa Morogoro.
Hivi sasa viwanda vya sukari vya Mtibwa na Ilovo kilichoko Kilombero pamoja na kile cha kutengeneza ngozi cha ACE, vimetozwa jumla ya sh. milioni 40 kwa makosa ya aina hiyo katika maeneo yao.
Uamuzi huo ulitolewa na Naibu Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira), Luhaga Mpina, akiwa katika mwendelezo wa ziara yake mkoani hapa  akiambatana na maofisa wa Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (Nemc).
Kiwanda cha Ilovo kimetozwa faini ya sh. m,ilioni 25 baada ya kubainika kuwa na mfumo mbovu wa utunzaji taka ngumu na kushindwa kuhifadhi vyema mabaki ya mabati yanayotolewa kiwandani hapo. Mbali na faini ambayo inatakiwa kulipwa ndani ya siku saba, walitakiwa kurekebisha upungufu huo ndani ya siku 30. 
Naibu waziri huyo aliutaka uongozi huo kuhakikisha upungufu 40 uliotajwa kwenye ripoti ya ukaguzi, iliyofanywa na Nemc zaidi ya miezi mitatu iliyopita, unafanyiwa marekebisho sambamba na kuutolea taarifa uwanja wa ndege ulioko ndani ya kiwanda hicho ambao hauna cheti chochote cha ukaguzi.
Kwa upande wa  kiwanda cha ngozi cha ACE cha mjini Morogoro, serikali imekitoza faini ya Sh. milioni 15 kutokana na kubainika kuwa na mfumo mbovu wa utiririshaji na uhifadhi wa maji taka.
Mpina pia aliiagiza menejimenti ya kiwanda kudhibiti  harufu mbaya inayolalamikiwa na wananchi, hususan walio jirani na kiwanda hicho.
Naibu Waziri Mpina alifanya ziara pia katika soko kuu la mjini Morogoro na kuagiza ujenzi mpya wa soko kuzingatia vizimba vya uhifadhi wa taka ili zisitawanyike na kuutaka uongozi wa manispaa kutofanya mlundikano wa taka katika eneo hilo kama ilivyoonekana.
Ziara hiyo ya Mpina iliyafikia pia maeneo ya kituo kikuu cha mabasi cha Msamvu, kiwanda cha kutengeneza mafuta ya kula cha Abood (Moproco), Kiwanda cha maturubai, Kiwanda cha nguo cha 21st  Century, Kiwanda cha Magunia na mabwawa yanayopokea majitaka yatokayo viwandani. 
Kutokana na maagizo ya Naibu Waziri, mtaalamu wa mazingira  kutoka Ilovo, Mary Kigula, alisema watahakikisha wanatekeleza ikiwa pamoja na kupanda miti na kutoa huduma za kijamii katika maeneo yanayowazunguka.
Naye Mkuu wa Idara ya Uzingatiaji wa Sheria ya mazingira kutoka Nemc, Alfred Msokwa, alisema baraza limekuwa likitoa ushauri na maelekezo kwa uongozi wa viwanda lakini wengi wamekuwa wakipuuza.
Msokwa alisema tangu mwaka 2013 NEMC imefanya ukaguzi katika  viwanda takribani vyote mkoani Morogoro na kutoa ushauri ambapo baadhi ya viwanda bado vipo katika utekelezaji wa marekebisho yake huku vingine vikipuuzia maelekezo hayo na kujikuta vikitakiwa kulipa faini kwa mujibu wa sheria.
CHANZO: NIPASH.

0 comments:

 
Supported by : Tone Media
Copyright © 2012. Morogoro Yetu - All Rights Reserved
Template Modify by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa