Home » » SOMA HAPA: UNDANI MTOTO ALIYEFICHWA UVUNGUNI MWA KITANDA

SOMA HAPA: UNDANI MTOTO ALIYEFICHWA UVUNGUNI MWA KITANDA


Stori: DUSTAN SHEKIDELE, MOROGORO
SAKATA la mtoto Devota Malole mwenye umri wa miaka mitano, ambaye ni mlemavu aliyeibuliwa baada ya kufichwa chini ya uvungu wa kitanda kwa muda wa miezi mitatu huko Matongolo, Dumila,Tarafa ya Magole wilayani Kilosa limeibua mambo mapya, baada ya kubaini kuwa aliyesababisha kuokolewa ni mume wa mama wa binti huyo.
Mtoto Devota Malole mwenye umri wa miaka mitano, ambaye ni mlemavu aliyeibuliwa baada ya kufichwa chini ya uvungu wa kitanda.
Mashuhuda waliokuwepo wakati wa kufichuliwa kwa mtoto huyo, wakiwemo majirani na wapangaji wa nyumba aliyokuwa akiishi, walisema mpangaji wa chumba hicho, Masumbuko Mkwama (25), aliishi peke yake kwa muda mrefu kabla ya miezi mitatu iliyopita, kuja na mwanamke aliyemzidi umri, Salah Mazengo (36) aliyemtambulisha kama mke wake akiwa na watoto watatu.
Msimamizi wa nyumba hiyo, Donata Sisie ambaye alidai mwenye nyumba anaishi Morogoro mjini, alisema baada ya kumuhoji mwanamke huyo, alisema alikuwa na watoto watano na kila mmoja alikuwa na baba yake na kwamba watatu kati yao, walichukuliwa na wazazi wao na hivyo kubaki na wawili, Elias mwenye umri wa miaka nane na mdogo wa mgongoni.
“Juzi Julai 8, Masumbuko aliwafuata wapangaji wenzake watatu na kuwaeleza kwamba mkewe ana mtoto mlemavu ambaye ni mgonjwa, lakini mwanamke huyo hataki mwanaye atibiwe, jambo ambalo linamshangaza. Kwa pamoja, watu hao walikwenda kutoa taarifa kwa Mwenyekiti wa Kitongoji, ambaye baada ya kuelezwa juu ya mtoto huyo, aliamua kwenda polisi.
Devota Malole akipata matibabu.
“Julai 10, mwaka huu, askari polisi pamoja na mwenyekiti huyo walikuja hapa nyumbani na kumfichua mtoto huyo chini ya uvungu. Tokea siku ya tukio, Masumbuko hajulikani alipo.
“Juzi ulitokea mvutano mkali hapa kwani mama mzazi wa Sala alifika akitaka kuchukuwa vyombo vilivyomo ndani ya chumba cha Masumbuko, mimi nilimzuia kwa hoja kwamba ninachojua chumba ni cha mvulana hivyo nimevichukua vitu vyake na kuvihifadhi kwangu hadi atakapofika.”

Mmoja wa wapangaji wenzake na Masumbuko, Asha Mohamed alisema alipohamia yeye na mumewe, walimkuta Masumbuko akiishi peke yake hadi miezi mitatu iliyopita walipomuona akimleta mwanamke mtu mzima aliyekuwa na watoto watatu, mmoja akiwa na ulemavu wa miguu.
Alisema alimuona mtoto mlemavu akiwa salama kwa siku moja tu, ile aliyofika na tangu hapo hakumuona tena.

.....akipewa msaada.
“Alipokuja alikaa naye hapa kwenye korido, sijamuona tena hadi juzi alipofichuliwa akiwa tofauti na nilivyomuona mwanzo, kiukweli huyo mtoto alizaliwa akiwa mlemavu na kwa mujibu wa maelezo ya mama yake, baba yake alimkana baada ya kumuona na ulemavu.
“Niwe mkweli kwenye hili, mtoto huyu alifichwa uvunguni tangu ahamie hapa, hii inatokana pengine na ugumu wa maisha kwani kwenye chumba chao wana kitanda futi nne na wanalala wanne baba, mama mtoto wao mkubwa Elias na huyo mtoto wa mgongoni, kuna kipindi nilimuuliza Devota alikuwa wapi aliniambia kuwa alimpeleka kwa bibi yake yaani mama yake anayeishi kitongoji kinachofuata,” alisema Asha.
Kwa upande wake, mwenyekiti wa kitongoji hicho, Dotto Hambosi alisema baada ya kupewa taarifa na wananchi wake aliwasiliana na polisi, ambao kesho yake walifika na kumkamata mwanamke huyo baada ya kukiri kuwa na mtoto uvunguni mwa kitanda chake. Baadaye walimpeleka Kituo cha Polisi Dumila kabla ya kumkimbiza katika Hospitali ya Wilaya ya Kilosa anakopatiwa matibabu.
Juu ya kazi za wazazi hao wawili, Hambosi alisema mwanaume anauza mishikaki na mwanamke pombe za kienyeji katika kilabu cha pombe za kienyeji


Chanzo: Global Publishers

0 comments:

 
Supported by : Tone Media
Copyright © 2012. Morogoro Yetu - All Rights Reserved
Template Modify by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa