Home » » 'HALMASHAURI MORO IONDOE DAMPO MAFISA'

'HALMASHAURI MORO IONDOE DAMPO MAFISA'

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 
 
HALMASHAURI ya Morogoro, imetakiwa kuondoa dampo la taka lililojengwa katika eneo la Mafisa,  kabla ya Desemba mwaka huu, kwani ni eneo la makazi ya watu.
Akizungumza katika ziara ya kushitukiza mbunge wa Morogoro Mjini, AbdulAziz Abood, alisema kutokana na kukua kwa mji dampo hilo kwa sasa linapaswa kuhamishwa kwa kuwa lipo jirani na makazi ya watu.
Abood alisema halmashauri hiyo ina eneo lingine lililopo nje ya mji katika kata ya Mkundi lililotengwa kwa ajili ya kutupa taka.
Alisema hatua ya kuwepo kwa dampo hilo katika makazi ya watu inaweza kuchangia kuwepo kwa magonjwa ya mlipuko ikiwemo kuharisha damu na kipindupindu.
“Nimesikia kilio cha wakazi hao ambacho ni cha muda mrefu na diwani wao amejaribu kila njia kutafuta muafaka wa suala hilo lakini bado kuna kigugumizi cha kuondoa dampo hilo,” alisema.
Alisema halmashauri hiyo ina uwezo wa kuhamisha dampo hilo kwa kuwa ina vitendea kazi vya kisasa yakiwemo magari ya kubeba taka.
Mbunge huyo alisema kuwa halmashauri haipaswi kuhofu gharama za kuhamisha dampo hilo kwa kuwa hatua ya kuendelea kumwaga taka katika eneo hilo ni sawa na kuweka rehani afya za wakazi hao.
Awali, wananchi wa eneo hilo walilalamikia hatua ya kuwepo kwa dampo hilo katika makazi yao kwani, limekuwa likichangia kuwepo kwa harufu mbaya ya uozo na nzi, huku pia wakilalamikia maji taka yanayomwagwa kutoka viwandani ambayo yanahatarisha usalama wa afya zao.
 chanzo :Tanzania Daima

0 comments:

 
Supported by : Tone Media
Copyright © 2012. Morogoro Yetu - All Rights Reserved
Template Modify by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa