Home » » RFE YASAIDIA MAKUNDI MOROGORO KWA BIL.36/-

RFE YASAIDIA MAKUNDI MOROGORO KWA BIL.36/-

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 
MFUKO wa Ufadhili wa Ukimwi (RFE), umetumia kiasi cha sh bilioni 36 kusaidia watoto yatima, wanaoishi na virusi na watu wanaotumia miili yao kibiashara.
Mwenyekiti wa Kamati ya Usimamizi wa mfuko huo, Profesa Saleh Muhammed, alieleza hayo juzi wakati wa ufunguzi wa mkutano wa kupitia utekelezaji wa miradi inayofadhiliwa na mfuko huo.
Alisema kiasi hicho cha fedha zaidi ya sh bilioni 36 kimetumika katika utekelezaji wa miradi mbalimbali ikiwa ni pamoja na taasisi 215 kupatiwa ufadhili kwa lengo la kusaidia jamii.
Kwa mujibu wa Profesa Muhammed, taasisi hizo ni pamoja na zinazojishughulisha na kuwajali na kuwasaidia watoto yatima na wanaoishi kwenye mazingira magumu, watu walio katika hatari zaidi ya kuambukizwa VVU kutokana na mazingira ya shughuli na tabia zao.
Aliyataja makundi hayo kuwa ni pamoja na wanaotumia miili yao kibiashara maarufu kwa jina la dada poa, wanaume wanaojamiiana na wenzao, madereva wa masafa marefu na watu wanaojidunga sindano zenye dawa za kulevya.
Alisema kutokana na taarifa ya Tume ya Taifa ya Kudhibiti Ukimwi (TACAIDS) na ile ya Zanzibar (ZAC) za hivi karibuni, kiwango cha maambukizi mapya ya VVU kinatofautiana kutoka mkoa mmoja hadi mwingine na yameripotiwa kupungua katika baadhi ya mikoa.
“Hali hii imetokana na kazi kubwa inayofanywa na serikali kuu, halmashauri zetu na asasi zisizo za serikali kwa ushirikiano wa karibu na asasi mbalimbali, ikiwa ni pamoja na nchi zenye ubalozi hapa nchini na Umoja wa Mataifa,” alisema.
Alisema tathmini iliyofanywa kwa pamoja na TACAIDS na ZAC kwa ufadhili wa Shirika la Maendeleo la Uswisi Mwaka 2009 kuhusu utendaji kazi na ufanikishaji wa shughuli za RFE, imeonyesha mfuko huo una umuhimu katika mapambano dhidi ya ugonjwa huo.
Meneja Mradi wa Kanisa Anglikana Dayosisi ya Mara, Rhobi Samwel, alisema RFE imewawezesha kiasi cha sh milioni 198 walizozitumia kuelimisha jamii.
Alisema Serengeti kuna tatizo la ukeketaji ambao wazazi wanalazimisha watoto hadi leo kuwafanyia ukatili huo, hivyo wamekuwa wakitoa elimu kwa wazazi kuwataka waache.
Chanzo:Tanzania Daima

0 comments:

 
Supported by : Tone Media
Copyright © 2012. Morogoro Yetu - All Rights Reserved
Template Modify by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa