Home » » Wananchi Dumila ‘walilia’ makazi

Wananchi Dumila ‘walilia’ makazi

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 

Waathirika wa mafuriko eneo la Dumila mkoani Morogoro wameiomba Serikali kuharakisha kuwapatia makazi ya kudumu ili waweze kuendelea na shughuli zao kama ilivyokuwa awali.
Wakizungumza jana kwa nyakati tofauti waathirika hao kutoka vijiji vya Mateteni na Magole walisema bado wanaishi katika mazingira magumu hali inayowasababisha kushindwa kufanya shughuli mbalimbali za kiuchumi ikiwamo kilimo.
Mwenyekiti wa Kambi ya Mateteni, Mustafa Choteka aliiomba Serikali kuwahurumia waathirika hao kwa kuharakisha kuwapatia nyumba za kudumu kwa kuwa wanaishi katika mazingira magumu.
“Tunaishukuru Serikali na taasisi mbalimbali ikiwamo Chama cha Msalaba Mwekundu, wametusaidia mahitaji mbalimbali, lakini bado kuna haja ya kutuweka katika sehemu salama,”alisema Choteka.
Hata hivyo, Rais wa Chama cha Msalaba Mwekundu Tanzania, Dk. George Nangale alitoa wito kwa waathirika hao kuanza kutayarisha mashamba yao ili waweze kuwa na chakula cha kutosha huku wakisubiri makazi ya kudumu.
“Serikali iharakishe kuwasaidia waathirika hawa kwani bado wapo katika hali ngumu, hivyo ni vyema wakipewa maeneo ya kudumu waliyoahidiwa mapema ili waweze kuendelea na maisha yao ya kawaida,” alisema Dk.Nangale
Alisema Chama cha Msalaba Mwekundu kimeweza kutoa misaada ya magodoro, vyombo, nyumba za muda (matenti) na vijana wa kujitolea kukaa na waathirika hao kwa kipindi hiki ili kuwawapatia ushauri nasaha.
Mkuu wa Mkoa wa Morogoro, Joel Bendera alisema tayari Serikali za vijiji hivyo wameshatoa viwanja kwa waathirika wa mafuriko.
“Hivi ninavyokuambia Serikali za vijiji hivi wameshaanza kuwagawia viwanja vya kujenga nyumba zao, sisi kazi yetu ni kuwahudumia lakini kujenga nyumba ni wao wenyewe”alisema Bendera.
Bendera alisema tangu waathirika hao wakumbwe na adha ya mafuriko Serikali inaendelea kuwahudumia kwa kuwapa chakula na mahitaji mengine.
“Tutaendelea kutoa mahema mapya kwa yale yanayovuja na chakula tutatoa hadi hapo wanakijiji hao watakapovuna mazao yao,”alisema.
Chanzo;mwananchi

0 comments:

 
Supported by : Tone Media
Copyright © 2012. Morogoro Yetu - All Rights Reserved
Template Modify by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa