Home » » Misaada yazidi kumiminika Magole

Misaada yazidi kumiminika Magole

OFISI ya Waziri Mkuu Kitengo cha Maafa imetoa tani 105 za mahindi na vifaa vingine kwa ajili ya watu walioathiriwa na mafuriko katika Tarafa ya Magole, wilayani Kilosa.
Pia imetoa magodoro na mabati kwa ajili ya watu hao waliokumbwa na mafuriko Januari 22 mwaka huu.
Mkuu wa Mkoa wa Morogoro, Joel Bendera alitoa taarifa hiyo juzi katika kituo cha Dakawa, Kilosa, kunakohifadhiwa vyakula na vifaa vya misaada kwa ajili ya wananchi wa vijiji vya Kata Dumila, Msowero, Berega na Magole.
Bendera alisema taarifa ya awali, inaonesha walioathiriwa na mafuriko kwa wilaya ya Kilosa, Gairo na Mvomero ni watu 12,472. Kati yao hao watu 12,010 ni kutoka Tarafa ya Magole wilayani Kilosa.
“Takwimu hizi bado ni za awali tulizomwambia Rais alipofika kuwapa pole waathirika wa mafuriko na kutembelea eneo lote lililokumbwa na mafuriko,” alisema.
Alisema kwa sasa wanakamilisha kwa kuwaainisha walengwa kwa kuwaandika majina yao, idadi ya watu kwenye kaya na wale waliobomokewa na nyumba zao na kukosa mahala pa kuishi ili misaada iwafikie moja kwa moja.
Katika hatua nyingine, Mkurugenzi Mtendaji wa Kampuni ya Yono Auction Mart, Scholastika Kevela amekabidhi vyakula vyenye thamani ya zaidi ya Sh milioni 1.5 kwa waathirika wa Tarafa ya Magole.
Wakati huo huo, Serikali imepanga kuhamisha Shule ya Msingi Magole wilayani Kilosa, ilipo sasa katika eneo linalokumbwa na mafuriko ya mara kwa mara kwa kujenga majengo mapya sehemu salama zaidi.
Mkuu wa Wilaya ya Kilosa, Elias Tarimo, alisema hayo juzi mbele ya Wajumbe wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Maendeleo ya Jamii, iliyoongozwa na Mwenyekiti wake, Said Mtanda ilipotemebelea Magole kwa ajili ya kutoa pole na kusikiliza shida zao.
Wajumbe wa Kamati hiyo walikagua majengo ya Shule ya Msingi Magole, nyumba za walimu na jengo la Mahakama ya Mwanzo, ambayo yote yaliathiriwa na mafuriko.
Chanzo;Habari Leo

0 comments:

 
Supported by : Tone Media
Copyright © 2012. Morogoro Yetu - All Rights Reserved
Template Modify by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa