Home » » Wakulima kuboresha zao la tumbaku

Wakulima kuboresha zao la tumbaku

WAKULIMA wa zao la tumbaku nchini, wameahidi kuongeza juhudi za kulifanya liwe bora zaidi ikiwa ni pamoja na kulitunza, kulichambua na kuondoa uchafu kabla ya kuliuza, ili lifikie viwango vya ubora wa kimataifa.
Hayo yalibainishwa jana na baadhi ya wakulima wa zao hilo kutoka wilaya za Mlele na Mpanda mkoani Katavi, walipofanya ziara ya mafunzo kwenye Kiwanda cha Kusindika Tumbaku Tanzania (TTPL) cha mjini Morogoro.
Wakulima hao wametoka kwenye vyama vitatu vya ushirika vya msingi ambavyo ni Ilunde kilichocho Kata ya Inyonga wilayani Mlele na vyama vya msingi vya Mishamo na Katumba vilivyopo wilayani Mpanda.
Wakizungumza wakati wa ziara hiyo, walisema wameshuhudia uchafu wa aina mbalimbali kama manyoya ya ndege, kokoto, vipande vya plastiki  ukiondolewa kwenye tumbaku kabla ya kusindikwa  kiwandani.
Mwenyekiti wa Chama cha Msingi Mishamo, Pilidas Anacredo, alisema ziara hiyo imewafumbua macho hususani baada ya kugundua kazi ya kuisindika tumbaku inakuwa ngumu zaidi kiwandani pale ambapo inapokuwa imechanganywa na uchafu.
“Tusipoboresha zao hili, kwa kweli hatuwezi kulifikisha kwenye viwango vya ubora vya kimataifa ambako ushindani ni mkubwa, hivyo tunaporejea majumbani tutazidi kueneza ujumbe huu ili ufike mbali zaidi,” alisema.
Akizungumzia mafanikio anayoyapata kwenye tumbaku, alisema zao hilo analolima kwenye ekari 22 kila mwaka linamuingizia sh milioni 12, ambazo zimemsaidia kujenga nyumba bora na ya kisasa, kusomesha watoto kwenye shule nzuri na kumiliki magari.
Mkulima mwingine kutoka Chama cha Msingi Ilunde, Martin Mlonga alisema ziara hiyo imewafundisha mambo mengi ikiwemo kufahamu zaidi mfumo wa biashara ya tumbaku kuanzia usindikaji hadi uuzaji wake.
Maofisa wa TTPL waliwaasa wakulima hao kuliboresha zao hilo, kwani faida zake zina manufaa kwa wakulima, wanunuzi na taifa kwa jumla.
Mkurugenzi wa Sheria na Uhusiano wa Kampuni ya Tumbaku Tanzania Leaf Tobacco Company Limited (TLTC) ambaye pia ni mmoja wa wakurugenzi wa Kampuni ya Tanzania Tobacco Proceesors Limited (TTPL), Richard Sinamtwa alisema zao hilo linanufaisha wakulima hao na taifa kwa ujumla, hivyo ubora wake ni muhimu ili liweze kushindana kwenye soko la kimataifa.
“Kwa mfano kiwanda kinapokuwa kinafanya kazi zaidi ya watu 5000 hunufaika na ajira ya moja kwa moja hapa, TANESCO inalipwa zaidi ya shilingi milioni 300 kwa mwezi, manispaa inalipwa kodi mbalimbali ukiachia mbali serikali kuu inayolipwa kodi kutoka kwenye zao hili,” alisema.
Meneja wa Kilimo na Shughuli wa TLTC, Louis Rousos alisema lengo la ziara hiyo ni kuwaonyesha wakulima hao namna bora ya kulihudumia zao hilo kuanzia mashambani hadi ghalani na kujionea vionjo vya wateja.
Chanzo;Tanzania Daima

0 comments:

 
Supported by : Tone Media
Copyright © 2012. Morogoro Yetu - All Rights Reserved
Template Modify by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa