Home » » Halmashauri yatenga ekari 10 za makaburi

Halmashauri yatenga ekari 10 za makaburi

HALMASHAURI ya Manispaa ya Morogoro imetenga kiwanja namba 675 kitalu ‘E’ chenye zaidi ya ekari 10 kilichoko kata ya Tungi kwa ajili ya makaburi.
Utengaji wa kiwanja hicho umekuja baada ya eneo hilo kuvamiwa na matapeli kisha kuuza kinyemela.
Eneo hilo ambalo siku za karibuni limeamsha tafrani baada ya kujikuta likijengwa bila utaratibu na watu wanaodaiwa kuuziwa viwanja na matapeli, limemlazimu Mkurugenzi wa Manispaa  Jorvis Simbeye kumwagiza Ofisa Mtendaji Abuu Liwangila kata ya Tungi Liwangila kulilinda eneo hilo kwa shughuli hizo.
Kwa mujibu wa barua ya Ofisa Mtendaji kwenda kwa Mkurugenzi wa Manispaa, kiwanja hicho sasa kimepimwa kwa kuzingatia ramani ya mipango miji namba10/178/996 na kuidhinishwa na Mkurugenzi wa Mipango Miji na Vijiji nchini kupitia Wizara ya Ardhi na Nyumba na Maendeleo ya Makazi 3/3/1997.
“Pia ramani ya kiwanja hicho iliidhinishwa na  mkurugenzi wa ramani na upimaji Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi 26/07/2006…ofisi inakujulisha na kukuthibitishia kuwa eneo namba 675 kitalu ‘E’ Tungi ni kwa ajili ya matumizi ya kuzikia na si vinginevyo,” alifafanua Mtendaji kupitia barua hiyo.
Salumu Tonyoke mkazi wa Tungi alipongeza uamuzi huo wa manispaa akisisitiza kuendelea kusimamia vema maeneo ya wazi na shughuli maalumu kwa faida ya vizazi vya sasa na baadaye.
Mbali na hilo aliitaka serikali kuhakikisha inapima maeneo mapema na kuwagawia wananchi hata kwa mkopo ili kukomesha wimbi la makazi holela.
“Unajua watu wanalazimika kutapeliwa kiurahisi kutokana na mfumo mbovu wa kimaslahi binafsi uliojaa serikalini, viwanja vinapimwa vichache, vyote vinachukuliwa na madiwani na watendaji wa serikali ili waje wawauzie wananchi kwa bei ya kuwalangua, sasa wananchi hawana uwezo wa kununua bei zao wanaona ni bora wakanunue kwa mtu bila kujali lolote,” alifafanua Tonyoke.
Chanzo;Tanzania Daima

0 comments:

 
Supported by : Tone Media
Copyright © 2012. Morogoro Yetu - All Rights Reserved
Template Modify by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa