Home » » Wafugaji, wakulima wauana, wachoma kituo cha polisi

Wafugaji, wakulima wauana, wachoma kituo cha polisi

Watu watatu wanadaiwa kufariki dunia akiwemo askari polisi na wengine watatu kujeruhiwa kutokana mgogoro kati ya wakulima na wafugaji wa jamii ya Kisukuma katika Kijiji cha Igwati, Tarafa ya Malinyi wilayani Ulanga. 
Taarifa zilizopatikana kutoka eneo la tukio zimedai kuwa wakulima walivamia kituo cha polisi kwa lengo la kushinikiza wenzao watatu kuachiwa baada ya kukamatwa wakituhumiwa kumuua mfugaji aliyetambulika kwa jina la Matanyi Luchoma (16).  Ilidaiwa kuwa wananchi hao baada ya kupata taarifa za kukamatwa kwa wenzao walifika kituo cha polisi ambapo, hawakuwakuta watuhumiwa hao baada ya polisi kuwahamishia kituo kingine na hivyo kuamua kuchoma moto kituo hicho pamoja na gari la askari. Wananchi hao walifanya vurugu kituoni, ambapo yalitokea mapigano kati yao na polisi, hivyo kumuua askari mmoja na askari nao kuwaua wananchi wawili na kujeruhi wengine watatu. Kamanda wa Polisi Mkoa wa Morogoro, alipotafutwa kuthibitisha tukio hilo, simu yake ilikuwa haipatikani. Hata hivyo alipotafutwa Kaimu Kamanda wa Polisi, John Laswai, alikiri kutokea tukio hilo na kwamba Kamanda alikuwa eneo la tukio. Mgogoro huo unadaiwa kuanza Desemba 13, mwaka huu saa 2 usiku katika Kijiji cha Igwati Malinyi wilayani Ulanga ambapo kundi la wananchi lilimkamata mfugaji huyo mkazi wa Lupeleme na kumpeleka katika ofisi za kijiji cha Lugawa. Ilidaiwa kuwa baada ya kumfikisha kwenye ofisi hizo, mtendaji alimfungia mtuhumiwa ndani na kuanza kuhoji sababu ya wananchi kujichukulia sheria mkononi jambo ambalo halikuwapendeza, hivyo kuanza kumshambulia mtendaji huyo hadi akakimbia. Alisema walivunja ofisi na kisha kuanza kumpiga kijana huyo hadi kusababisha kifo chake. Hata hivyo ilidaiwa kuwa chanzo cha mauaji hayo kilisababishwa na baadhi ya watu wanaodaiwa kuwa wafugaji wa jamii ya Kisukuma kuvamia nyumbani kwa mjumbe wa kamati ya mazingira, Victoria Marietha, kisha kumpiga na kumsababishia majeraha. Mjumbe huyo alikimbizwa katika Hospitali ya Lugala, Tarafa ya Malinyi ambapo alifariki dunia wakati akipatiwa matibabu. 
Chanzo;Majira

0 comments:

 
Supported by : Tone Media
Copyright © 2012. Morogoro Yetu - All Rights Reserved
Template Modify by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa