Home » » Mgogoro wakulima, wafugaji waendelea

Mgogoro wakulima, wafugaji waendelea

WAKULIMA wa Wilaya ya Kiteto, Manyara, wameomba serikali iwape kibali cha kuwaondoa wafugaji kama yenyewe serikali imeshindwa kutatua mgogoro huo ambao umedumu kwa miaka mingi.
Wakulima walitoa kauli hiyo juzi muda mfupi baada ya kuvunjika kwa mkutano wa hadhara ulioandaliwa na wafugaji kwa ajili ya kupinga kauli ya Naibu Spika na mbunge wa Kongwa Job Ndugai (CCM) aliyesema viongozi wa Dodoma na Manyara wameshindwa kutatua mgogoro kati ya wakulima na wafugaji kutokana na kuwepo kwa vitendo vya ukabila.
Mkulima Iddi Shabani alisema wakulima wamechoshwa na vitendo vya unyanyasaji wanavyofanyiwa na wafugaji kwa kushirikiana na baadhi ya viongozi wa serikali.
Shabani alisema kutokana na kuwepo kwa mgogoro wa miaka mingi kati ya jamii ya wakulima na wafugaji wakati taarifa zikiwa zinawafikia viongozi  wameshindwa kutatua mgogoro huo sasa umefika wakati wa kuomba wapewe kibali cha kufanya vita kati ya wakulima na wafugaji.
“Mgogoro huu ni wa miaka mingi sasa tumekuwa tukiwaambia viongozi wa Dodoma na Manyara lakini hakuna kinachofanyika na sasa tunamuomba Waziri Mkuu afike eneo hili atusikilize… lakini kama hawezi basi tunamuomba rais afike watusikilize,” alisema.
Alisema kitendo cha wakulima kuendelea kufukuzwa na kunyanyaswa na kundi la wafugaji ni jambo linalosababishwa na ubaguzi wa kikabila unaofanywa na watendaji ndani ya serikali kwa kuwapendelea wafugaji ambao ni Wamasai na kuwanyanyasa wakulima.
“Tunashangazwa na serikali kuwapa kipaumbele wafugaji ambao kazi yao kubwa ni kufuata mikia ya ngo’mbe huku hata hawana mahali pa kuishi kwa maana ya kutokuwa na nyumba lakini wakulima wanaolisha nchi nzima wanaendelea kunyanyaswa jambo ambalo halikubaliki,” alisema.
Chanzo;Tanzania Daima

0 comments:

 
Supported by : Tone Media
Copyright © 2012. Morogoro Yetu - All Rights Reserved
Template Modify by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa