Home » » CHADEMA Kilosa wataka serikali kujitathmini

CHADEMA Kilosa wataka serikali kujitathmini

CHAMA cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) Wilaya ya Kilosa, kimefunga mwaka huku kikiitaka serikali wilayani humo kujipima na kujitathimini kama imefanikiwa kutawala kwa maendeleo.
Akizungumza katika mkutano uliofanyika mjini hapa juzi, Mwenyekiti wa CHADEMA Kilosa, Seleman Simba, alisema umasikini walionao wananchi unatokana na mfumo mbovu wa utawala ndani ya serikali.
Udhaifu huo alioutafsiri kuwa unatokana na kuogopana kinafiki kwa lengo la kulindana, ulisababisha maafa makubwa baina ya wananchi wilayani humo na kuendeleza wimbi la umasikini usiotarajiwa kutokana na hali ya hewa na ardhi.
“Ni nani hapa nchini na nje ya nchi hafahamu kuwa Kilosa ndiyo wilaya pekee ya mfano wa migogoro ya ardhi? Si chini ya watu watatu wanakufa kila wiki kutokana na migogoro hii, lakini nani na kwa mbinu gani ameshituka kukomesha hayo?” alihoji Simba.
Alisema nchi imejaa sheria za ardhi zisizotekelezeka, na kusisitiza kuwa sheria hizo zitaendelea kuchakaa kwenye makabati ya serikali hadi hapo nchi itakapopata viongozi kutoka vyama vingine ikiwemo CHADEMA.
Awali, Mhamasishaji wa Kanda, Shabani Dimoso, alisema bado serikali haijawa na dhamira ya kukomesha wizi na ufujaji wa mali na fedha za umma akitoa mfano kwenye halmashauri hiyo kuendelea kupata hati chafu.
“Wananchi wasiogope na kutishwa na mamlaka iliyopo kwa kuwa wanachopigania ni haki yao kikatiba,” alifafanua Dimoso.
Chanzo;Tanzania Daima

0 comments:

 
Supported by : Tone Media
Copyright © 2012. Morogoro Yetu - All Rights Reserved
Template Modify by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa