Home » » Kamati ya Bendera yaanza kuchunguza mauaji Moro

Kamati ya Bendera yaanza kuchunguza mauaji Moro

Ulanga. Mkuu wa Wilaya ya Ulanga, Francis Miti amesema kamati iliyoundwa na Mkuu wa Mkoa wa Morogoro, Joel Bendera kuchunguza chanzo cha vurugu zilizosababisha mauaji ya wakulima watatu wanaodaiwa kuuawa na polisi katika Kijiji cha Igawa, Kata ya Malinyi, Ulanga imeanza kufanya kazi na kwamba hali ya usalama na amani imerejea.
Akizungumza jana mjini hapa Miti alisema baada ya tume hiyo kukamilisha uchunguzi wake, wananchi watapewa taarifa ya chanzo cha vurugu hizo zilizotokea baada ya wananchi kuvamia Kituo cha Polisi Malinyi na kufanya uharibifu.
Alisema wakati kamati hiyo ikiendelea na kazi yake, Jeshi la Polisi limewahamisha baadhi ya askari wa kituo hicho akiwamo mkuu wake ili kuleta imani.
Mkuu huyo wa Wilaya alisema uamuzi wa kuwahamisha askari hao ulikuja baada ya baadhi ya wananchi, hususan wakulima kutokuwa na imani nao.
Alisema baada ya Kamati ya Ulinzi na Usalama ya Wilaya kufanya vikao na mikutano ya hadhara, wakulima na wafugaji walikubaliana na kuunda kamati ya pamoja kila upande ukiwa na wawakilishi watano ili kuimarisha amani na usalama.
Alisema hivi sasa wananchi wanaendelea na shughuli zao za kiuchumi na kijamii na kuwataka viongozi wa eneo hilo kuwa mstari wa mbele kurejesha amani badala ya kuchochea vurugu.
Chanzo;Mwananchi

0 comments:

 
Supported by : Tone Media
Copyright © 2012. Morogoro Yetu - All Rights Reserved
Template Modify by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa