Home » » Tibaijuka, Chiza, Mathayo wajitosa Mvomero

Tibaijuka, Chiza, Mathayo wajitosa Mvomero


MAWAZIRI watatu; Injinia Chritopher Chiza wa Kilimo, Chakula na Ushirika, Prof. Anna Tibaijuka wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi na Dk. Mathayo David wa Mifugo na Uvuvi, wamejitosa wilayani Mvomero mkoani Morogoro kutanzua mgogoro kati ya wafugaji na wakulima. Mapigano hayo yalitokea kati ya Novemba 5 na 6 mwaka huu na kusababisha vifo vya watu sita, huku wengine zaidi ya 50 wakijeruhiwa vibaya katika Kata ya Hembeti wilayani Mvomero.
Kwa mujibu wa diwani wa kata hiyo, Juma Malaja, mawaziri hao walitarajia kupokea taarifa mbalimbali kutoka kwa wananchi juu ya mgogoro huo na nini kifanyike ili kuumaliza.
Alisema kabla ya mkutano na wananchi katika kijiji hicho cha Hambeti, mawaziri hao walitarajia kukutana na kamati ya ulinzi na usalama ya wilaya chini ya mkuu wa wilaya hiyo, Anthon Mtaka, kwa taarifa fupi ya maendeleo na hatima ya mapigano hayo.
Hata hivyo, wakati viongozi hao wakijaribu kutafuta muafaka wa tatizo hilo kwa kuwakutanisha wafugaji na wakulima, Jeshi la Polisi na viongozi wa serikali wilaya na mkoa, wanadaiwa kuhusika katika vurugu hizo.
Madai hayo ya viongozi kuhusika yalikanushwa na Kamanda wa Polisi Mkoa wa Morogoro, Faustine Shilogile, akisema ni maneno ya wapita njia.
Kwa mujibu wa Diwani Mjala, jioni ya Novemba 4, wanakijiji walikamata ng’ombe wasiopungua 300 wakiwa wameharibu chanzo cha maji na kula mazao ya watu mbalimbali mashambani.
Alisema kuwa alipopewa taarifa za kukamatwa kwa mifugo hiyo, alitoa taarifa kwa OCD na mkuu wa wilaya hiyo, akiomba msaada zaidi wa kiulinzi ili waimarishe ulinzi kutokana na tabia za wafugaji zilivyo, kuwa kungeibuka mapigano muda wowote.
“Baada ya kukamatwa kwa ng’ombe wale, mimi niliamua kutoa taarifa kwa viongozi wa juu, lakini pia kuomba kuongezewa nguvu ya ulinzi maana kama wanavyofahamika wafugaji, wasingevumilia mifugo yao ilale nje, lakini mpaka Novemba 5, hakuna askari aliyekuwa amefika,” alisema Malaja.
Aliongeza kuwa saa 12 jioni ya Novemba 6, walipelekwa askari ambao hawakufanya lolote kutokana na mazingira ya mapambano kuwa magumu kutokana na aina ya silaha zilizokuwa zikitumika na muda kuwa umeisha.
Vurugu hizo zilizimwa na Kamishina wa Operesheni Makao Makuu, Paul Chagonja aliyeingia eneo la tukio huku watu sita wakiwa wamepoteza maisha na wengine wengi kujeruhiwa vibaya.

Chanzo;Tanzania Daima

0 comments:

 
Supported by : Tone Media
Copyright © 2012. Morogoro Yetu - All Rights Reserved
Template Modify by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa