MAMLAKA ya Uendelezaji wa Bonde la Mto Rufiji (RUBADA) imewataka
maofisa ugani katika Halmashauri ya Wilaya ya Morogoro Vijijini kuwa
wabunifu katika utendaji wao ili kuongeza thamani ya mazao pamoja na
kutoa elimu stahiki kwa wananchi wanaowatumikia.
Mkurugenzi Mkuu wa RUBADA, Aloyce Masanja, alitoa ushauri huo katika
Halmashauri ya Wilaya ya Morogoro, mkoani hapa wakati wa semina elekezi
kwa watendaji wa halmashauri hiyo juu ya mpango wa serikali wa Matokeo
Makubwa Sasa (BRN) hivi karibuni.
“Ni vema maofisa ugani wakaelewa kuwa wao ndio viongozi katika suala la kutoa maelekezo kwa wananchi wao,” alisema.
Alisema maofisa ugani waliopo ni wachache kulinganisha na mahitaji
yaliyopo katika vijiji, hivyo kazi kubwa iliyopo ni kujaribu kuwapa
elimu ili waendane na mfumo uliopo na mahitaji ya wakati.
“Tumekuwa na wagani wachache katika vijiji, japo wanafanya kazi
lakini wamekuwa si mfano bora kwa wale wanaowatumikia, kutokana na wao
wenyewe kutojishughulisha na kilimo na ndiyo maana hata wananchi
wamekuwa na hamasa ndogo juu ya suala la kilimo,” alisema Masanja.
Aliongeza kuwa utakuta ofisa ugani hana shamba au mfugo, jambo
linalosababisha wao wenyewe kutokuwa na mwamko katika sekta ya kilimo
na mifugo katika vijiji wanavyofanyia kazi.
Akizungumzia upungufu wa maghala ya chakula katika Wilaya ya Morogoro
Vijijini, Masanja alisema tatizo hilo linatokana na kuwepo kwa maghala
ya zamani ambayo hayana viwango vya kuweza kuhifadhi chakula.
“Katika mpango wa Matokeo Makubwa Sasa tunataka kila kijiji kiwe na
kilimo cha umwagiliaji na patajengwa ghala la kisasa kwa ajili ya
kuhifadhia chakula,” alisema.
Alisisitiza kuwa sasa kuna upotevu mkubwa wa chakula hasa mpunga na
mahindi kutokana na kutohifadhiwa katika maeneo maalumu, hivyo
kusababisha njaa zisizokuwa za lazima katika maeneo kadhaa ya wilaya
hiyo.
Mkuu wa Wilaya ya Morogoro Saidi Amanzi, alisema serikali ina nia
nzuri ya kuwakomboa wananchi wake kiuchumi, hivyo ni vema wakaunga
mkono juhudi zinazofanywa na serikali yao.
“Sisi upande wa serikali tunajitahidi kutoa elimu kwa wananchi juu ya
suala la kilimo chenye tija na kitakachomkomboa mwananchi,” alisema
Amanzi.
Chanzo;Tanzania Daima
0 comments:
Post a Comment