Home » » Mwenyekiti anusurika kuuawa

Mwenyekiti anusurika kuuawa

MWENYEKITI wa Serikali ya Mtaa wa Lugala maarufu kama machimbo ya mchanga mweupe mjini Morogoro, Willison Mizola (CHADEMA), amenusurika kufa baada ya kuvamiwa na kupigwa na watu aliodai kuwa wafuasi wa Chama Cha Mapinduzi (CCM).
Akizungumza kwa tabu na mwandishi wa habari katika Hospitali ya Rufaa mkoani Morogoro alipolazwa kwa matibabu, Mizola ambaye ni mwenyekiti pekee katika Manispaa ya Morogoro kupitia upinzani, alisema tukio hilo lilitokea Novemba 28 wakati akielekea kwa rafiki yake Mtaa wa Lugala, Kata mpya ya Mindu.
Alisema siku ya tukio, akiendesha pikipiki katika maeneo ya korongo jirani na machimbo hayo, alizingirwa na kundi la watu wakiwa na aina mbalimbali za silaha za jadi kisha kumpiga nazo sehemu za mwili jambo lililomsababishia kupoteza fahamu na kuanguka chini.
“Waliponiona nakuja, nikasikia wakisema kwa sauti ‘huyo ndiye tunayemtafuta muda mrefu sasa amepatikana’.
“Pale kulikuwa na mitambo ya kupakilia mchanga kwenye magari, na miongoni mwa waliokuja kinishambulia ni pamoja na wale wenye mtambo huo,” alisema Mizola.
Alisema baada ya kuona amepoteza fahamu, watu wale hawakutaka kuchukua ile pikipiki ila walimpora sh 1,360,000 alizokuwa akirejesha kwa mdeni wake.
“Baada ya muda nilizinduka na kufanikiwa kuinua pikipiki na kuiwasha kisha nikaondoka eneo hilo hadi kwa rafiki yagu niliyekuwa naenda kwake ambaye alinikimbiza kituo cha polisi na kupata PF3 kwa ajili ya matibabu,” alisema.
Mizola alisema kuwa aliambiwa kuwa mishipa miwili ya damu shingoni imefyatuka na kuyumba.
Aliwataja baadhi ya vijana aliowatambua kuhusika na tukio hilo kuwa ni Komu Adam, Omary, Torati Mathias, Athuman Malolo, Elistini Msumle, Israel Mganda na Victor Mkude wote wakazi wa Mtaa wa Lugala.
Kamanda wa Polis Mkoa wa Morogoro, Faustin Shilogile amethibitisha kutokea kwa tukio hilo na kwamba Mizola amefungua jalada la shambulio namba MOR/IR/6697/13 na IR/12981/13 lakini hadi sasa hakuna aliyekamatwa.
Chanzo;Tanzania Daima

0 comments:

 
Supported by : Tone Media
Copyright © 2012. Morogoro Yetu - All Rights Reserved
Template Modify by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa