Home » » MAKALA: TAWA ILIVYOFANIKIWA KUIMARISHA ULINZI WA RASILIMALI YA WANYAMAPORI NCHINI

MAKALA: TAWA ILIVYOFANIKIWA KUIMARISHA ULINZI WA RASILIMALI YA WANYAMAPORI NCHINI

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 





Mamlaka ya Usimamizi wa Wanyamapori Tanzania (TAWA) ni mamlaka iliyoanzishwa kwa Amri ya Serikali na kutangazwa kwenye gazeti la Serikali Na.135 la tarehe 9 Mei, 2014. Uanzishwaji wa Mamlaka hii ni utekelezaji wa kifungu cha 8 cha Sheria ya kuhifadhi Wanyamapori Na. 5 ya mwaka 2009.
Mamlaka ya Wanyamapori imeanza kazi rasmi tarehe 1 Julai,2016 na Makao Makuu  kwa sasa yapo hapa Morogoro katika eneo la Taasisi ya Utafiti wa mazao ya Misitu (TAFORI).
TAWA inasimamia Mapori ya Akiba 28, Mapori Tengefu 42, maeneo manne (4) ya Ardhioevu yanayotambuliwa na Mkataba wa kimataifa wa Ramsar pamoja na maeneo ya wazi yenye wanyamapori. Aidha, TAWA ni muangalizi wa shughuli za uhifadhi wanyamapori kwenye maeneo ya Jumuiya za Uhifadhi za Wanyamapori kwa jamii (Wildlife Management Areas).
Mamlaka inatekeleza majukumu yake kwa kuzingatia Sera ya Wanyamapori ya mwaka 2007, Sheria ya Uhifadhi Wanyamapori Na. 5 ya mwaka 2009 na kanuni zake. Vilevile, Mamlaka inatekeleza mikataba ya kimataifa ya uhifadhi wa wanyamapori pamoja na mazingira yao ambayo Tanzania imeridhia. Mamlaka kwa kushirikiana na Taasisi nyingine za uhifadhi wa Wanyamapori na Misitu inatekeleza Mkakati wa kupambana na Ujangili na biashara haramu ya nyara za Serikali wa miaka mitano (2014-2019).
Mamlaka ilianzishwa kama chombo cha utekelezaji wa majukumu  kwa niaba ya Serikali chini ya uangalizi wa Serikali na  kuwa na mfumo unaonesha utekelezaji wa majukumu kwa ufanisi zaidi. Kama ilivyo kwa Mamlaka nyingine nchini, lengo la kuanzishwa kwa TAWA, ni kutekeleza majukumu ya Idara ya Wanyamapori hasa ya Usimamizi wa Wanyamapori nchini. Ikiwa ni pamoja na kusimamia shughuli za utawala, ulinzi na usimamizi wa raslimali ya Wanyamapori katika maeneo yote nje ya Hifadhi za Taifa na eneo  ya Ngorongoro. Hii ni pamoja na kutekeleza kazi zifuatazo;
Kusimamia Mapori ya Akiba na Mapori Tengefu, Kusimamia na kulinda shoroba za wanyamapori, maeneo ya mtawanyiko, ardhioevu, na maeneo ya wazi yenye wanyamapori, Kuangalia Usimamizi wa wanyamapori katika Maeneo ya Jumuiya ya Hifadhi za Wanyamapori, Mashamba na Bustani za wanyamapori kwa mujibu wa miongozo inayotolewa na Mkurugenzi wa Wanyamapori.
Kusimamia migogoro kati ya wanyamapori na binadamu kwa kushirikiana na wadau wengine wa uhifadhi, Kushirikiana na sekta binafsi pamoja na wananchi katika kuanzisha na kusimamia uwekezaji katika maeneo ya wanyamapori, Kutoa, kurejea au kufuta vibali vya matumizi ya wanyamapori, Kusimamia himasheria na kukabili ujangili. Kueleimisha wadau kuhusu thamani ya  wanyamapori.
Kushirikisha wadau katika kuhifadhi na kunufaika na raslimali ya wanyamapori nchini, Kushiriki katika Utekelezaji wa mikataba ya kikanda na kimataifa Kusimamia masuala ya utawala bora katika Usimamizi wa wanyamapori na Kuendeleza na kujenga uwezo wa Mamlaka katika Usimamizi wa wanyamapori.
Moja ya sababu ya kuanzishwa TAWA ni uwezo mdogo wa utendaji wa idara ya wanyamapori uliotokana na uchache wa rasilimaliwatu, fedha na vitendea kazi.
Mafanikio
Katika kipindi cha Julai 2016 hadi Octoba 2017, Mamlaka iliendelea kuimarisha Ulinzi wa rasilimali ya Wanyamapori ndani na nje ya Mapori ya Akiba, Mapori Tengefu na maeneo ya Ardhioevu (Ramsar Sites). Muundo wa usimamizi na ulinzi wa rasilimali za wanyamapori katika Mamlaka umegawanywa katika makundi makuu mawili. kundi la kwanza linahusisha mameneja wanaosimamia mapori ya akiba 28 na “Ramsar Sites” 3; na kundi la pili ni wakuu wa kanda 8 wa Kikosi Dhidi Ujangili (KDU).
Mamlaka inashirikiana na Halmashauri za Wilaya na Jumuiya za Hifadhi za Wanyamapori (WMAs) katika ulinzi na usimamizi wa wanyamapori kwenye mapori Tengefu, maeneo ya wazi na udhibiti wa wanyamapori hatari kwa maisha ya binadamu na waharibifu wa mali za wananchi.
Kiujumla TAWA imefanikiwa kutekeleza mambo yafuatayo
Kuimarisha usimamizi wa rasilimali za wanyamapori na kuboresha uwezo wa kukusanya maduhuli, Mamlaka imeendeleza mfumo wake wa kukusanya mapato kwa kutumia mfumo wa kielektronic ili kupunguza mianya ya upotevu wa mapato.
Kutokana na mabadiliko ya mfumo wa kiraia kwenda mfumo wa kijeshi .TAWA imeanza  kuendesha mafunzo ya maandalizi ya kuingia Jeshi usu (Paramilitary) katika kambi ya Mlelele iliyoko Katika Pori la Akiba Rukwa/Lwafi Mkoani Katavi. Mafunzo haya pia yanashirikisha askari kutoka Hifadhi za Taifa na Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro. Tangu mafunzo haya yaanze tumeshapeleka Askari zaidi ya 260 ambao wameshahitimu na sasa sasa hivi kuna askari 60 wanaendelea na mafunzo hayo.
TAWA kupitia Serikali ya awamu ya Tano chini ya Mhe. Rais Dkt John Pombe Joseph Magufuli, imeendelea kukabiliana na ujangili kwa nguvu zote kwa njia mbalimbali ikiwa ni pamoja na kutekeleza Mkakati wa kupambana na ujangili na biashara haramu ya nyara za Serikali (National Antipoaching Strategy to Combat Poaching and Illegal Wildlife Trade) iliyozinduliwa Novemba, 2014.
Doria  na intelijensia ndani na nje ya maeneo yaliyohifadhiwa zinaendelea kufanyika nchi nzima.
Serikali kwa kushirikiana na  jumuiya za kimataifa zikiwemo taasisi za kikanda na kimataifa, imefanya jitihada mbalimbali kukabiliana na ujangili wa tembo. Zimeonekana dalili za kupungua kwa ujangili wa tembo nchini kutokana na jitihada kubwa ya kuimarisha doria za kupambana na ujangili hali hiyo imesaidia kukamatwa kwa silaha nyingi zilizokuwa zikitumika kwa ujangili.
Jumla ya watuhumiwa 2,053 walikamatwa kwa makosa mbalimbali na kufunguliwa mashitaka ambapo jumla ya kesi 859 zilifunguliwa. Kesi 10 + 126 zenye watuhumiwa 248 zilihukumiwa kifungo cha jumla ya miezi 8,295 na kesi 198 zenye watuhumiwa 234 watuhumiwa walilipa faini jumla ya shilingi 387,985,063/=.
Nyara za aina mbalimbali zilikamatwa katika kipindi cha kuanzia Julai 2016 hadi Oktoba 2017 kama ifuatavyo; Meno ya tembo vipande 848 vyenye uzito wa kilo 2,664.48,  Nyamapori yenye uzito wa kilo 7,790 za spishi mbalimbali na Meno 8 ya kiboko, magunia 67 ya magamba ya kakakuona, ngozi 16, na mikia 33 ya wanyamapori mbalimbali.
Mwezi Julai,2016 kilianzishwa Kikosi Kazi kiitwacho’ Wildlife and Forest Crime Unit – WCU’ kinachosimamiwa na Watendaji wa Sekta ya Wanyamapori kupitia Kanda za Kiikolojia tisa, (Tasking and Coordination Groups – TCGs) ili kukabiliana na majangili katika ngazi za juu za uwezeshaji (Facilitators) ambacho kinashirikiana na vyombo vingine vya ulinzi na usalama kupitia Muungano wa Kitaasisi.
TAWA inaamini kwamba changamomoto za ujangili na uvunaji haramu wa misitu na matatizo mbalimbali yanayohikabili uhifadhi nchini hayawezi kutatuliwa kwa mfumo wa utendaji kazi wa kiraia. Hivyo, Wizara inakamilisha taratibu za kubadili mfumo wa utendaji kazi kutoka wa kiraia kwenda jeshi usu.
Mabadiliko haya ya kimfumo ni matakwa ya Sheria ya Uhifadhi Wanyamapori Na.5 ya mwaka 2009 ambayo imeanisha kwamba kutaundwa kikosi cha jeshi usu (Wildlife Protection Unit), ili kuhakikisha ulinzi kamili wa rasilimali katika maeneo yaliyohifadhiwa.
Katika kipindi cha mwezi Agosti hadi Oktoba, 2016 kikosi kazi hiki, kimefanikiwa kukamata majangili  107, kesi 9 ziko mahakamani, Aidha, nyara, silaha, vifaa mbalimbali  vya kufanyia ujangili vimekamatwa.
Ukaguzi wa nyara umeimarishwa katika viwanja vya ndege na bandari kwa kutumia mbwa maalum wa kunusa ili kutambua nyara na kufuatilia majangili.
Doria imeendelea kufanyika kwa kutumia ndege zisizotumia marubani ‘Drons’ kukabiliana na ujangili.
Elimu ya uhifadhi ni nyenzo muhimu katika kupambana na ujangili pamoja na uharibifu wa mazingiara. Mamlaka kwa kutambua umuhimu wa dhana nii, imetoa elimu ya uhifadhi kwa vijiji (45) vinavyozunguka Pori la Akiba Selous, vijiji (19) kuzunguka Pori la Akiba Rungwa/ Muhesi/Kizigo ,Tengefu na maeneo ya wazi ambayo ni vitalu vya uwindaji wa kitalii.
Aidha, wananchi walielimishwa  kwa njia ya runinga,redio,magazeti na kugawa vipeperushi kwa wananchi katika maonesho ya Sabasaba, nane nane, siku ya utalii duniani,siku ya tembo, siku ya wanyamapori duniani na siku ya ardhioevu duniani. Majarida 585, Vipeperushi 7000, Stickers 3000, Mabango 5 yenye ujumbe wa uhifadhi vimegawiwa kwa wananchi.
Ushirikishwaji wa jamii katika uhifadhi wa Wanyamapori uliimarishwa kwa kutangazwa eneo la Jumuiya la Hifadhi ya Wanyamapori (Wildlife Management Area-WMAs) Ngorongo, Utete na Mwaseni (JUHIWANGUMWA) lililoko katika Wilaya ya Rufiji mkoa wa Pwani lilitangazwa kwenye Gazeti la Serikali (GN. Na 204 la tarehe 01/07/2016) na kufanya jumla ya maeneo yaliyotangwazwa kuwa 22.
Kushirikiana na nchi jirani (Cross border collaboration) kutanzua changamoto za uhifadhi, ujangili na biashara haramu. Katika eneo hili Tanzania inashirikiana na Msumbiji, Zambia, Uganda na Kenya kukabili ujangili unaovuka mipaka ya nchi.Hivyo, Kutokana na hali mizoga ya tembo imeonekana na meno ya tembo kukamatwa.
Changamoto
Mamlaka ya Wanyamapori bado ni Mamlaka mpya. Mamlaka  katika kufanya kazi zake imekuwa na changamoto mbalimbali zikiwemo za ujangili,mwamko mdogo wa Watanzania kutembelea vivutio vya utalii ikiwemo mapori ya akiba; ubovu wa miundombinu katika maeneo yaliyohifadhiwa, shughuli za kibinadamu hususan kilimo na uingizaji wa ng’ombe katika katika maeneo yaliyohifadhiwa na matumizi haramu ya wanyamapori.
Ujangili na biashara haramu ya meno ya tembo
Bado imeendelea kuwa changamoto  ya kiuhifadhi. Hali hii inaathiri siyo tu kuuawa kwa wanyamapori, bali pia inahatarisha utalii na usalama wa nchi yetu. Sensa ya mwaka 2014 iliyofanyika nchi nzima ilionyesha kwamba idadi ya tembo nchini ni 43,330 ikionyesha kupungua kwa idadi ya tembo kutoka tembo 109, 051 mwaka 2009, Sawa na asilimia 60.3% ya kupungua kwa idadi ya tembo katika kipindi cha miaka mitano. Pia matokeo ya sensa ya mwaka 2014 yalionyesha ongezeko la asilimia 16% la idadi ya tembo katika mfumo wa Ikolojia wa Selous-Mikumi kwa kufikia 15,217 kutoka 13,084 iliyokuwa mwaka 2013. (Chanzo:Sensa za TAWIRI.)
Mapito/Shoroba za Wanyamapori
Zinaendelea kuzibwa na uvamizi wa mifugo/shughuli za binadamu katika maeneo yaliyohifadhiwa. Hali hiyo imesababisha kuongezeka kwa migogoro baina ya binadamu na wanyamapori na kupungua kwa idadi ya wanyamapori hususani tembo ndani na nje ya maeneo yaliyohifadhiwa.







 

0 comments:

 
Supported by : Tone Media
Copyright © 2012. Morogoro Yetu - All Rights Reserved
Template Modify by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa