Home » »
Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 

Mwalimu wa serikali agundulika kulipwa mishahara miwili

Mkuu wa Mkoa wa Morogoro, Dk Stephen Kebwe
MWALIMU wa Shule ya Sekondari Masagati inayomilikiwa na serikali katika Halmashauri ya Wilaya ya Kilombero Mkoa wa Morogoro, Justian Julias amegundulika kuajiriwa mara mbili, ikiwamo katika shule nyingine binafsi na kuendelea kulipwa mishahara miwili kwa nyakati tofauti.
Mwalimu huyo amebainika na wajumbe wa timu ya mkoa ya uhakiki wa kina kwa watumishi hewa iliyoundwa na Mkuu wa Mkoa wa Morogoro, Dk Stephen Kebwe.
Julias ni mwalimu wa Shule ya Sekondari Masagati ya serikali na katika uhakiki wa kina aligundulika akiwa na ajira nyingine katika shule binafsi ya Mbingu wilayani Kilombero.
Timu hiyo ilipita katika halmashauri zote za mkoa huo kufanya uhakiki wa kina kuanzia Mei 12 hadi Julai 12, mwaka huu na jumla ya watumishi batili 315 waliobainika katika uchunguzi huo na Halmashauri ya Wilaya ya Kilosa ikiongoza kwa watumishi hewa 98 ikifuatiwa na Mji wa Ifakara kwa watumishi hewa 48.
Mkuu wa mkoa huyo alisema hayo kwa waandishi wa habari jana kwenye kikao cha kujadili utekelezaji wa maagizo ya Makamu wa Rais, Samia Suluhu Hassan kuhusu kutenga maeneo ya malisho na kutumia fursa hiyo kutoa taarifa ya watumishi hewa na kukamilishwa kwa zoezi la uhakiki wa kina katika halmashauri zote nane za mkoa huo.
“Mwalimu huyo analipwa mishahara miwili na waajiri wawili tofauti...nimeagiza hatua za kisheria zichukuliwe kwa mkuu wa shule na mwalimu mwenyewe na taarifa zake ziwasilishwe kwangu mara moja,” alisisitiza Dk Kebwe.
Dk Kebwe aliunda timu ya watu saba ya uhakiki wa kina watumishi hewa kutoka vyombo vya ulinzi na usalama na Sekratarieti ya Mkoa iliyoongozwa na Mwenyekiti Marieta Njovu, ambayo imebaini fedha zilizolipwa kutokana na watumishi hao hewa ni Sh 2,213,997,780.78. Kati ya hizo, zilizokwisha rejeshwa serikalini ni Sh 42,762,779.98.
Chanzo Na Habari Leo

0 comments:

 
Supported by : Tone Media
Copyright © 2012. Morogoro Yetu - All Rights Reserved
Template Modify by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa