Home » » Ashikiliwa na Polisi kwa kujifanya daktari

Ashikiliwa na Polisi kwa kujifanya daktari

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Morogoro, Ulrich Matei
POLISI mkoani hapa inamshikilia mtu mmoja aliyetambuliwa kwa jina ya Zakaria Benjamin Migomba (35) mkazi wa Tungi, Manispaa ya Morogoro, kwa tuhuma za kuingia isivyo halali katika hospitali ya rufaa ya mkoa wa Morogoro na kujifanya kuwa ni daktari.
Kamanda wa Polisi wa mkoa huu, Ulrich Matei alisema tukio hilo lilitokea Julai 10, mwaka huu, saa 10: 00 alfajiri ambako mtuhumiwa huyo aliingia katika hospitali hiyo kwa nia ya kutenda kosa.
Alisema mtuhumiwa huyo alitembelea wodi mbalimbali ikiwemo namba moja na namba tisa na alipofika wodi namba saba, alienda moja kwa moja eneo la chumba cha kubadilisha nguo na kuchukua koti la daktari na kulivaa.
Kwa mujibu wa Kamanda Matei, baada ya kuchukua koti na kulivaa alikwenda moja kwa moja wodi ya wagonjwa mahututi ambapo alipofika wodini hapo muuguzi wa zamu alimshtukia na kuiarifu Polisi juu ya mtu huyo.
Kamanda alisema askari walipopata taarifa hiyo walifika mara moja hospitalini hapo na kumkuta mtuhumiwa huyo na alipohojiwa alidai kuwa yeye ni daktari mgeni alikuwa akitembelea wagonjwa ili kukagua na kuona kama wanapatiwa huduma ipasavyo.
“Tayari alikuwa ametembelea wodi kadhaa ikiwemo namba moja, tisa na saba ambapo alichukua koti la daktari na kulivaa akijifanya kuwa yeye ni daktari mgeni hivyo anakagua wagonjwa kuona kama wanapatiwa huduma ipasavyo,” alisema Kamanda Matei.
Hivyo alisema baada ya kukamatwa alipohojiwa na kufanyika uchunguzi wa awali ilibainika kuwa yeye si daktari wala mfanyakazi wa hospitali hiyo na kwa sasa anashikiliwa kwa uchunguzi zaidi kutokana na kauli zake kuwa yeye ni askari mpelelezi na pia kuona iwapo akili yake iko sawa.
Kwa upande wake, mtuhumiwa huyo alijitambulisha kuwa ni Zakaria Benjamin Migomba kutoka Gairo na kwamba elimu yake ni darasa la saba.
Inaelezwa kuwa wakati huo huo alitoa maelezo yanayojichanganya kuwa ni askari wa jeshi la kujitegemea aliyefika hospitalini hapo kufanya kazi ya Rais, jambo lililowapa wasiwasi juu ya utimamu wa akili yake.
Chanzo Na Habari Leo

0 comments:

 
Supported by : Tone Media
Copyright © 2012. Morogoro Yetu - All Rights Reserved
Template Modify by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa