Home » » WAENDESHA BODABODA WAPIGWA WAKIHUSISHWA NA WIZI

WAENDESHA BODABODA WAPIGWA WAKIHUSISHWA NA WIZI

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 

WATU watatu wakiwemo waendesha bodaboda wawili wamenusurika kifo baada ya kupata kipigo kutoka kwa wananchi wakituhumiwa kupora mkoba wa mwanamke.
Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Morogoro, Ulrich Matei alisema tukio hilo ni la juzi saa moja asubuhi katika eneo la Msamvu, Manispaa ya Morogoro.
Kamanda Matei alitaja waliotambulika kwa jina moja moja ni Makhirikhiri (mwendesha pikipiki) na Ngasa ambao wote ni wakazi wa Misufini. Mwingine hakutambuliwa mara moja.
Alisema wakiwa na pikipiki yenye namba za usajili MC 436 AVX aina ya Sanlg, walipora mkoba wa Pendo Wilson (30), mkazi wa Msamvu akiwa njiani kwenda kazini kwake.
Alisema mwanamke huyo alipiga kelele za kuomba msaada na ndipo watu walioshuhudia tukio, walianza kufuatilia vijana hao kwa pikipiki na kuwakamata walipofika maeneo ya Modeco-Ipoipo.
Kamanda Matei alisema wananchi wenye hasira walianza kushambulia kwa magongo na mawe na kuwasababishia majeraha sehemu mbalimbali za mwili. Watuhumiwa hao waliokolewa na polisi waliofika eneo la tukio baada ya kupata taarifa za tukio. Waliwahishwa Hospitali ya Rufaa ya mkoa wa Morogoro kupata matibabu.
Kufuatia vitendo vya uhalifu vinavyofanywa na madereva bodaboda, Kamanda Matei alisema polisi itaendelea kusaka wahalifu ambao baadhi yao wanatoka nje ya mkoa na kujihusisha na biashara za bodaboda, lakini wakijihusisha na matukio ya uhalifu.
Amewataka viongozi wa vyama vya waendesha bodaboda kukagua wanachama wao kwa kuwasajili watambulike maeneo wanayofanyia kazi zao na iwe rahisi kuwatambua. Alitoa mwito kwa wananchi kuacha tabia ya kujichukulia sheria mkononi wanapowakamata wahalifu ni vyema watoe taarifa polisi.
Chanzo Gazeti la Habari leo
 


0 comments:

 
Supported by : Tone Media
Copyright © 2012. Morogoro Yetu - All Rights Reserved
Template Modify by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa