Home » » Tanesco kuunganisha wateja wapya 11,300

Tanesco kuunganisha wateja wapya 11,300

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 

WAKATI Serikali ikielekeza nguvu zake katika mapinduzi ya uchumi kupitia viwanda, mkoa wa Morogoro umejiweka katika nafasi nzuri ya kunufaika kutokana na kuongezeka kwa kasi ya miradi ya umeme.
Tayari Shirika la Umeme Nchini (TANESCO) liko kwenye hatua za mwisho za kumalizia miradi mikubwa ya umeme, ukiwamo mradi wa umeme mijini na ule unaofadhiliwa na Wakala wa Umeme Vijijini (REA) ambapo zaidi ya watu 11,300 wanatarajiwa kunufaika.
Akizungumza jana ofisini kwake, Mhandisi wa umeme wa Tanesco mkoani Morogoro, anayeshughulikia masuala ya ujenzi, David Chisot alisema kupitia miradi hiyo, wateja wakubwa na wadogo watafikiwa na nishati ya umeme katika maeneo ambayo awali hayakuwa na umeme kabisa.
Alisema wananchi hao watapata fursa ya kuanzisha viwanda vidogo na vikubwa katika maeneo yenye fursa ya malighafi za uzalishaji, wananchi kujiajiri na kuongeza ajira kwa wengine na kufanya maendeleo mengine yanayohitaji nishati ya umeme katika maeneo yao.
Chisot alifafanua kuwa miradi inayofadhiliwa na Rea itahusisha wilaya nne za mkoa wa Morogoro ikiwemo Morogoro katika vijiji 27, Mvomero vijiji 35, Kilombero vijiji vinne na Ulanga vijiji vitano ambapo tayari wateja 5,562 wa mradi wa Rea wameanza kunufaika na mpango huo wakiwamo wateja wadogo 5,457 na wakubwa 205.
Alisema, “Kuna miradi mipya 69 inayogharimu Sh bilioni nane inayotekelezwa, katika hiyo miradi 18 imekamilika, 28 wakandarasi wapo maeneo ya kazi wakiendelea na ujenzi na 23 haijaanza huku miradi 38 ikiwa ni endelevu na kati yake 10 tayari imekamilika na 12 haijakamilika, lakini wakandarasi wanaendelea na umaliziaji”.
Alisema katika utekelezaji wa miradi hiyo, changamoto mbalimbali zimeendelea kujitokeza, ikiwamo watu kudai fidia pale wanapokwenda kuweka nguzo za umeme katika nyumba au wanapopitisha nyaya za umeme katika maeneo ya makazi na wengine kufanya uharibifu wa kukata miti na kuwafanya kukosa umeme wakisingizia Tanesco ndio waliokata umeme huo.
“Naomba niweke wazi kuwa umeme wa Rea haina fidia, kuna maeneo tulishapita na kuweka njia, lakini ukirudi kwenye kazi unakuta nyumba zimezuia, hii inatuathiri sana, lakini inawaathiri wananchi ambao ndio wafaidika wakubwa wa umeme,” alisisitiza Chisot.
Aidha, amewasihi wananchi kuacha kuwatumia vishoka au njia zisizostahili hasa pale wanapohitaji huduma ya umeme na kuwataka wafuate njia sahihi ikiwemo kufika ofisi za Tanesco kwa maelekezo juu ya kupata huduma za shirika.
Chisot aliwashauri wateja ambao tayari wamefikiwa na huduma hiyo waisaidie Tanesco kwa kufunga nyaya katika nyumba zao ili iwe rahisi kufungiwa umeme, lakini akawaonya wateja kutojiunganishia umeme kutoka kwa mafundi wasio rasmi ambao hawatambuliki na shirika hilo.
Kwa upande wao, wananchi wa Morogoro wameelezea matumaini yao juu ya mpango huo wa Tanesco, ambapo baadhi yao Issaya Kennedy, Lucas Simon na Marietha Kitaly walisema hatua hiyo ni nzuri na itasaidia kuharakisha maendeleo.
Chanzo Gazeti La Habari Leo

0 comments:

 
Supported by : Tone Media
Copyright © 2012. Morogoro Yetu - All Rights Reserved
Template Modify by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa