Home » » RC AAGIZA PICHA ZA ANGA KUWEZESHA UPIMAJI ARDHI

RC AAGIZA PICHA ZA ANGA KUWEZESHA UPIMAJI ARDHI

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 

Mkuu wa Mkoa wa Morogoro, Dk Stephen Kebwe

MKUU wa Mkoa wa Morogoro, Dk Steven Kebwe ameziagiza halmashauri zote mkoani kwake kununua picha za anga ili mpango wa upimaji ardhi unaofanywa na mradi wa kuwezesha umilikishaji ardhi (LTSP) mkoani hapa uweze kuwa wa kisasa zaidi.
Akifungua mkutano wa mawasilisho ya mpango wa matumizi ya ardhi wa Wilaya ya Kilombero, Dk Kebwe alisema kwamba ili mradi wa LTSP uweze kuwa wa manufaa, ni lazima halmashauri zinunue picha hizo. Mradi huo unatekelezwa katika wilaya za Kilombero, Ulanga na Malinyi.
“Gharama za satellite image (picha za anga) ni kati ya Sh milioni 80 na 100, naziagiza halmashauri zote kuhakikisha kwa mwaka huu zinanunua satellite image ili tuweze kupima ardhi yetu kisasa zaidi kuliko utaratibu huu tunaotumia sasa ni wa kizamani zaidi,” alisema Dk Kebwe.
Dk Kebwe alisema picha hizo zitasaidia halmashauri kutambua ardhi na majengo yaliyopo katika maeneo yao na kutoza kodi. Alisema halmashauri ziache visingizio vya kutokuwa na pesa za kununua picha hizo hadi kusubiri fedha za wahisani wa maendeleo.
Katika hotuba yake, mkuu huyo wa mkoa alisema upimaji huo wa ardhi utasaidia kuondoa migogoro ya ardhi katika mkoa wake na akaonya kuwa wale wote ambao wana mashamba makubwa katika mkoa wake na hayajaendelezwa yatachukuliwa na kugawiwa kwa watu ambao wana matatizo ya ardhi.
Aliwahakikishia kuwa barabara ya kutoka Kidatu kwenda Ifakara mjini itajengwa kwa kiwango cha lami kwani tayari Umoja wa Ulaya umeshatoa fedha za kujenga barabara hiyo. Alisema upimaji wa ardhi ukikamilika na barabara ikajengwa wilaya ya Kilombero, Ulanga na Malinyi zitapiga hatua kubwa kwa maendeleo.
Kiongozi wa timu ya urasimishaji ya ardhi wa LTSP Swagile Msananga, mradi huo awali ulikuwa utekelezwe katika wilaya ya Ulanga na Kilombero, lakini baada ya Ulanga kugawanywa na kuzaliwa wilaya mpya ya Malinyi nayo imewekwa kwenye mradi huo.
Alisema lengo la mradi huo ni kupima kila kipande cha ardhi kilichoko katika wilaya hizo na kuwapa hati miliki za ardhi pamoja na hati miliki za kimila kwa wananchi waishio maeneo ya vijijini.
Mradi wa uwezeshaji wa kumiliki ardhi (LTSP) chimbuko lake ni kuimarisha ushirikiano kati ya Tanzania na nchi za kundi la G8 kuhusu uwazi katika sekta ya ardhi. Mpango huo unafadhiliwa na nchi za Uingerea, Denmark na Sweden.

Chanzo Gazeti la Habari leo
 

0 comments:

 
Supported by : Tone Media
Copyright © 2012. Morogoro Yetu - All Rights Reserved
Template Modify by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa