Home » » Mkwasa aagiza watumishi wazembe kutumbuliwa

Mkwasa aagiza watumishi wazembe kutumbuliwa

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 

Mkuu wa Wilaya ya Mvomero, Betty Mkwassa.
MKUU wa Wilaya ya Mvomero, mkoani Morogoro, Betty Mkwasa, amemwagiza Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya hiyo, kuchukua hatua za haraka kwa watumishi waliosababisha jengo la vyumba vitatu vya madarasa katika Shule ya Sekondari Wami kushindwa kutumika.
Jengo hilo lilijengwa kwa gharama ya zaidi ya Sh milioni 300 na limebainika kujengwa kwa kiwango cha chini na limejengwa kwa ufadhili wa fedha za Mfuko wa Maendeleo ya Jamii (Tasaf). Mkwasa alisema ukaguzi ulipofanyika ulibaini limejengwa chini ya kiwango na wanafunzi kushindwa kutumia kutokana na ubovu huo wa zaidi ya miaka mitatu sasa.
Alitoa agizo hilo alipotembelea shule hiyo mwishoni mwa wiki kwa ajili ya kukagua shughuli za kitaaluma, mpango wa kumaliza changamoto ya madawati, vyumba vya madarasa na vyoo. Katika ziara hiyo alijionea jengo hilo la vyumba vitatu vya madarasa likiwa halitumiki kutokana na nyufa nyingi ukutani na sehemu ya paa kuezuliwa na upepo.
Mkwasa pia aliagiza apatiwe taarifa ndani ya siku tatu kuanzia Machi 10 mwaka huu, kwa nini jengo hilo limejengwa chini ya kiwango wakati majengo mengine shuleni hapo yamejengwa kwa ubora.
Alishangaa kwa nini uongozi wa halmashauri haujachukua hatua kwa waliohusika na jambo hilo kwa kusababisha uwepo wa upungufu wa vyumba vya madarasa na kuwafanya idadi kubwa ya wanafunzi kurundikana madarasani.
“Jengo hilo limejengwa chini ya kiwango na hatua hazijachukuliwa, na haiwezekani kukarabatiwa wakati waliosababisha wapo na hawajachukuliwa hatua hadi sasa” alihoji Mkwasa.
Naye Mkuu wa shule hiyo, Lupyana Kissiya, alisema wakati akihamia shule hiyo mwaka 2013, alilikuta jengo hilo la vyumba vitatu limekamilika lakini bila kutumiwa na wanafunzi kutokana na kubainika kuwa ni bovu baada ya ya ukaguzi kugundua limejengwa chini ya viwango.
Alisema ripoti ya ukaguzi uliofanywa na Idara ya Elimu Sekondari wilayani humo, ilibaini hayo na kueleza kuwa jengo hilo halifai kwa matumizi ya wanafunzi kwa kuwa linahatarisha usalama wao.
Kissiya alisema Idara ya Elimu ya Sekondari ilipendekeza mkurugenzi mtendaji wa halmashauri afahamishwe kwa barua, ambapo alimtuma mhandisi wa ujenzi kulifanyia ukaguzi na mhandisi alipendekeza likarabatiwe lakini ukosefu wa fedha umefanya lisikarabatiwe hadi sasa
 
Chanzo Habari leo

0 comments:

 
Supported by : Tone Media
Copyright © 2012. Morogoro Yetu - All Rights Reserved
Template Modify by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa