Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399.
Mkuu wa Wilaya ya Kilosa Mhe. John Henjewele akifungua mafunzo ya uboreshaji wa daftari la kudumu la wapiga kura yaliyofanyika Juni 5, 2015 Katika Ukumbi wa Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Morogoro. Kulia, ni Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Kilombero Bi Azimina Mbilinyi.
Baadhi ya wajumbe wa mafunzo hayo wakila kiapo cha uaminifu katika utekelezaji wa zoezi ambalo liko mbele yao. Kushoto ni Hakimu Mkazi Bi. Agnes Ringo.
Bi. Sajira Mbaga ambaye ni Afisa kutoka tume ya Taifa ya Uchaguzi, akihojiwa nawaandishi wa habari mara baada ya ufunguzi wa mafunzo hayo.
Baadhi ya vifaa vilivyowasili Mkoani Morogoro kwa ajili ya zoezi la uboreshaji wa daftari la kudumu la wapiga kura.
Picha na Andrew Chimesela
Na Andrew Chimisela
Mkoa
wa Morogoro umeanza maandalizi ya uboreshaji wa daftari la kudumu la
wapiga kura kwa ajili ya uchaguzi Mkuu wa Wabunge na Rais wa Jamhuri ya
Muungano wa Tanzania unaotarajiwa kufanyika Mwezi Oktoba mwaka huu.
Maandalizi
hayo yameanza jana kwa semina ya siku mbili inayotolewa kwa waratibu wa
uboreshaji wa daftari la kudumu la wapiga kura katika ngazi ya Mkoa na
Wilaya za Mkoa wa Morogoro.
Semina
hiyo inalenga kutoa Elimu itakayowawezesha kutekeleza jukumu hilo
katika kufanikisha zoezi hilo muhimu. Mafunzo hayo yatahusisha ujazaji
wa fomu zitakazotumika kwenye zoezi zima la uboreshaji la wapiga kura.
Aidha,
yatatolewa mafunzo kwa vitendo yatakayohusu jinsi ya kutumia kifaa cha
kisasa yaani Biometric Voters Registration (BVR) kinachochukua alama
mbalimbali za mpiga kura kwa lengo la kuondoa uwezekano wa mtu
kujiandikisha zaidi ya mara mbili.
Akifungua
mafunzo hayo Mkuu wa Mkoa wa Morogoro Dkt. Rajabu Rutengwe kupitia
hotuba iliyosomwa na Mkuu wa Wilaya ya Kilosa Mhe. John Henjewele,
aliwataka wanasemina kujifunza kwa bidii na kuhakikisha wanajua
utaratibu unaotakiwa kutumika katika kuboresha daftari hilo la kudumu la
wapiga kura.
Dkt.
Rutengwe alitumia nafasi hiyo kuwaomba wananchi wa Mkoa wa Morogoro
kujiandikisha katika vituo vyao mara muda utakapowadia wa kufanya hivyo.
“Naomba kutoa wito kwa wananchi walio na sifa ya kuwa wapiga kura
Mkoani hapa waweze kujitokeza ili wajiandikishe”. Alisema.
“Aidha,
napenda kuwahakikishia kwamba Serikali Mkoani hapa imedhamiria
kuhakikisha zoezi hili linafanyika kwa ufanisi mkubwa na kufanikiwa”
Dkt. Rutengwe aliongeza.
Naye
Bi. Sajira Mbaga, Afisa kutoka Tume ya Uchaguzi alisema, zoezi la
kujiandikisha kwenye daftari la kudumu la wapiga kura kwa Mkoa wa
Morogoro, linatarajiwa kuanza kufanyika Juni 14 mwaka huu na kuongeza
kuwa Tume hiyo inaendelea na jitihada za kuondoa changamoto
zilizojitokeza kwenye zoezi hili katika Mikoa mingine ambapo zoezi hili
limekwisha fanyika.
0 comments:
Post a Comment