Home » » RC Morogoro aagiza sheria zitumike kupendezesha Manispaa

RC Morogoro aagiza sheria zitumike kupendezesha Manispaa

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 


indexNa. Andrew Chimesela – Morogoro
 
Mkuu wa Mkoa wa Morogoro Dkt. Rajab Rutengwe ameuagiza uongozi wa Halmashauri ya Manispaa ya Morogoro kutumia sheria zilizopo katika kusimamia vema suala la usafi wa mazingira.
 
Dkt. Rutengwe ametoa agizo hilo jana (19 Mei, 2015) wakati wa kikao maalum cha uhamasishaji wa kampeni ya kitaifa ya usafi wa mazingira kilichofanyika katika ofisi za mkoa huo.
 
Kiongozi huyo wa  ngazi ya mkoa alibainisha kuwa zipo baadhi ya sheria ambazo ni nzuri  na endapo zitafanya kazi mji wa Morogoro utakuwa safi  muda wote kwani sheria hizo zinaelekeza kila mwananchi kufanya usafi katika eneo analoishi.
 
“Kila mwananchi anatakiwa kufanya usafi wa mazingira umbali wa mita kumi kila upande kutoka eneo analoishi, yaani mbele ya eneo lake, nyuma, kushoto na kulia kwa eneo lake, sheria, taratibu na kanuni za usafi zisimamiwe kikamilifu” alisema. 
Aidha, Dkt. Rutengwe alikwenda mbali zaidi ya kampeni ya Kitaifa ya Usafi wa mazingira na kutaka juhudi zaidi zifanyike ili kung’arisha mji wa Morogoro hasa Manispaa ya Morogoro kwa kuwa Halmashauri hiyo ndio uso wa mkoa wa Morogoro.
 
’’Ndugu wadau, Mimi ninaheshimu sana mashindano haya lakini nimeona tuende zaidi ya mashindano ya usafi kwa kulenga mambo makuu yafuatayo;
Kuufanya mji wa Morogoro kuwa kijani wakati wote (Greening), Kuupendezesha mji wa Morogoro wakati wote (Beutification) na Kuwa na uendelevu wa usafi baada ya mashindano”, Dkt. Rutengwe alisisitiza.
Katika hatua nyingine Dkt. Rutengwe amewaomba Wanahabari Mkoani humo kutumia taaluma yao kuwaelimisha wananchi umuhimu wa usafi wa mazingira na hivyo kuuboresha mji wa Morogoro huku akiwataka Wasanii ambao ni wazawa wa mkoa huo nao wabuni na kutunga nyimbo zinazohamasisha, kuboresha na kutangaza vivutio vilivyoko katika Mkoa wa Morogoro.
 
Naye Mstahiki Meya wa Halmashauri ya Manispaa ya Morogoro Mhe. Amir Nondo, alisema katika kuendeleza Usafi wa mazingira wa Manispaa ya Morogoro muda wote, kuna sheria ndogo ambazo wanazitumia.
 
Nondo alibainisha kuwa moja ya sheria hizo ni kutoza faini ya shilingi elfu hamsini (Sh. 50,000/=) kwa kila mwananchi anayekamatwa akichafua mazingira kwa namna yoyote na faini hiyo anatozwa wakati huo huo.
 
Aidha, alisema wanatoa motisha ya shilingi elfu ishirini na tano (Sh. 25,000/=) kwa mwananchi yeyote atakayesaidia kukamatwa kwa wanaovunja sheria zilizopo na kuchafua mazingira ya halmashauri hiyo,
 
Awali, wakati akimkaribisha Mkuu wa Mkoa kwenye kikao hicho, mbele ya wadau wa usafi wa mazingira Ofisa Afya wa Mkoa wa Morogoro Bwana Carle Lyimo alisema, lengo la kikao hicho ilikuwa ni kutoa mrejesho kwa viongozi wa Mkoa kazi zilizofanyika kwenye Kampeini ya Usafi wa Mazingira katika Mkoa wa Morogoro na kuongeza ushiriki kwa viongozi pamoja na jamii katika utekelezaji wa Kampeini hiyo.
Aidha, kikao hicho kililenga kujadili mikakati ya namna ya kuboresha usafi katika maeneo mbalimbali ya Mkoa ili ifikapo wakati wa maadhimisho ya usafi kitaifa Mkoa uweze kushika nafasi ya juu kitaifa.
 Kwa Mkoa wa Morogoro Halmashauri zote zimekuwa zikishiriki kwenye mashindano hayo isipokuwa Halmashauri ya Manispaa ya Morogoro na Halmashauri ya Wilaya ya Gairo ambazo zimeanza kushiriki kwenye mashindano hayo mwaka 2014/2015.
Takwimu zinaonesha Halmashauri ya Manispaa ya Morogoro imekuwa na rekodi nzuri katika mashindano hayo hususani miaka ya hivi karibuni kama inavyooneshwa hapa chini mwaka na nafasi iliyoshika kwenye mabano;
Mwaka 2007 ilishika nafasi ya 18 kati ya Halmashauri 20, 2008 (15), 2009 (15), 2010 (12), 2011 (7), 2012 (12), 2013 (3) na 2014(3). mwaka 2015?
Kampeni ya Kitaifa ya Usafi wa Mazingira ilizinduliwa na Mhe. Rais wa Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete tarehe 5 Juni mwaka 2012 lengo likiwa kuboresha miundo mbinu ya usafi wa mazingira katika ngazi ya kaya na shule ili kuweza kufikia malengo ya kitaifa na kimataifa ambapo mashindano hayo ya Usafi Kitaifa yanatarajiwa kufanyika tarehe 5 Juni mwaka huu.

0 comments:

 
Supported by : Tone Media
Copyright © 2012. Morogoro Yetu - All Rights Reserved
Template Modify by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa