Home » » MAONI: SUALA LA MATUMIZI YA EFD LISICHUKULIWE KISIASA

MAONI: SUALA LA MATUMIZI YA EFD LISICHUKULIWE KISIASA

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 
 
 
Tangu Katibu Mkuu wa CCM, Abdulrahman Kinana na timu yake waanze ziara ya kikazi katika baadhi ya mikoa wiki iliyopita, wamesikika wakitoa kauli katika mikutano ya hadhara ambazo zimechukuliwa na baadhi ya wananchi kwamba zinaidhoofisha Serikali ya chama hicho. Wengi wamediriki kusema kwamba hali hiyo imejenga picha kwamba kauli za viongozi hao zinaonyesha kuwapo mvutano kati ya viongozi wa Serikali na chama hicho tawala, kwani hali kama hiyo imekuwa ikijitokeza pindi sekretarieti ya chama hicho inapofanya ziara katika sehemu mbalimbali nchini na kuhutubia mikutano ya hadhara.
Itakumbukwa kuwa, sekretarieti hiyo ilipofanya ziara ndefu mikoani miezi kadhaa iliyopita, tulishuhudia mikutano yake ya hadhara ikielekeza mashambulizi dhidi ya mawaziri wa Serikali. Pamoja na kuwaita baadhi ya mawaziri ‘mizigo’ na kumtaka Rais Jakaya Kikwete awafukuze kazi kwa kile viongozi hao walichokiita utendaji mbovu katika kutatua kero za wananchi, tulishangaa kuona tuhuma hizo dhidi ya mawaziri hao zikitolewa hadharani kwa mtindo ulioonekana kuwadhalilisha. Baadhi ya mawaziri walilalamikia kitendo hicho na huenda Rais Kikwete alisikiliza kilio chao kwa kuwa waliendelea na nafasi zao za uwaziri.
Ni katika muktadha huo, baadhi ya wananchi wanasema hotuba nyingi zinazotolewa sasa na viongozi wa sekretarieti hiyo walio katika ziara ya mikoa mbalimbali, ikiwamo Pwani na Tanga zinaichonganisha Serikali na wananchi. Maudhui ya hotuba nyingi wanazotoa hayalengi kuwaeleza na kuwaelimisha wananchi kuhusu hatua zinazochukuliwa na Serikali ya chama hicho katika kutatua matatizo yao, bali hotuba hizo zimetawaliwa na lawama, malalamiko na hasira dhidi ya Serikali ambayo imeundwa na chama chenyewe. Katika mkutano wa hadhara uliofanyika Chalinze, mkoani Pwani juzi, kwa mfano, katibu mkuu huyo wa CCM alihoji utaratibu aliouita mbovu wa matumizi ya mashine za kielektroniki za kutunza hesabu za wafanyabiashara (EFD), akisema bei ya mashine hizo ni kubwa na kuna upungufu katika sheria inayohusu matumizi ya mashine hizo.
 Huku akisema baadhi ya malalamiko ya wafanyabiashara ni ya msingi na yanapaswa kushughulikiwa, alisema wanaopinga matumizi hayo wako sahihi kabisa, huku akisisitiza kwamba kuna upungufu katika sheria inayohusu matumizi ya mashine hizo, hivyo wafanyabiashara wanaopinga matumizi yake wasionekane kama wakorofi. Alisema watu wanapopinga matumizi ya mashine hizo wanaambiwa wanavunja sheria wakati sheria yenyewe imepinda. Hata hivyo, swali la kujiuliza ni kwa nini chama hicho hakikuchukua hatua ya kuondoa udhaifu huo?
Sisi hatuna ugomvi na kauli hiyo kama ambavyo tumekuwa hatuna ugomvi na kauli zake nyingine ambazo yeye na timu yake wamekuwa wakizitoa katika mikutano ya hadhara. Ugomvi pekee tulionao ni kauli hizo kutolewa katika mikutano ya hadhara ambayo inaweza kusababisha baadhi ya wafanyabiashara kugoma kutumia mashine hizo kwa kauli hizo. Moja ya majukumu ya chama tawala popote duniani ni kutunga na kusimamia sera mbalimbali na kuhakikisha Serikali inazitekeleza. Pale inaposhindwa kufanya hivyo, chama tawala huchukua hatua stahiki, siyo kupitia katika mikutano ya hadhara ambapo watu hutaka kuambiwa tu yale wanayotaka kusikia.
Sisi tunaamini kuwa kila mfanyabiashara anapaswa kulipa kodi na tungependa suala la EFD lisichukuliwe kisiasa, ila wataalamu waachwe wafanye kazi yao bila kuingiliwa na wanasiasa.
 Chanzo;Mwananchi

0 comments:

 
Supported by : Tone Media
Copyright © 2012. Morogoro Yetu - All Rights Reserved
Template Modify by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa