Home » » WATOTO MORO WAHITAJI ULINZI ZAIDI

WATOTO MORO WAHITAJI ULINZI ZAIDI

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 

WATOTO wanaoishi katika mazingira magumu katika Manispaa ya Morogoro, wameandamana mjini hapa wakishinikiza kupatiwa ulinzi wa kutosha.
Watoto hao walitoa ombi hilo juzi, baada ya maandamano ya kuadhimisha Siku ya Haki ya Mtoto.
Walisema wanashangazwa na usimamizi wa sheria zilizopo licha ya nchi kutunga na kuridhia mikataba mingi ya kimataifa yenye mwelekeo wa kuwalinda.
Mmoja wa watoto hao, Veronica Omari, alisema wamechoshwa na taarifa mbaya dhidi yao zisizotafutiwa ufumbuzi wa kudumu ikiwemo kuwakamata na kuwahukumu watu wanaoendeleza vitendo viovu, jambo ambalo linawasababishia unyonge.
“Watoto tunauawa, tumekuwa chombo cha kukidhi haja za kimwili kwa watu wazima wakiwemo ndugu zetu, ushirikina na yote haya yanafanyika kwa kuwa hatuna wa kututetea kwa kuwa serikali haitujali… tunaomba serikali itutengenezee mazingira bora ya usalama na hadhi zetu,” alisema Veronica.
Akizungumza kwa niaba ya Kamanda wa Polisi Mkoa wa Morogoro, mwakilishi wake, Clemence Matata kutoka dawati la kupinga unyanyasaji wa kijinsia na ukatili kwa watoto, aliwataka watoto kufunguka kwa kutoa taarifa kwa jeshi hilo na watakuwa tayari kuwalinda na kuwatetea.
Awali waratibu wa hafla hiyo akiwemo Mratibu Mkuu wa Ustawi wa Jamii, Amani Center, Elly Maarifa na Mkurugenzi Mtendaji wa World Vision Tanzania, Rehema Mwbwala kwa niaba ya asasi ya kimataifa ya Save Family Tanzania Charity (SFTC), waliiomba serikali kuzitekeleza sheria na mikataba ya watoto ambayo Tanzania imeridhia.
Chanzo:Tanzania Daima

0 comments:

 
Supported by : Tone Media
Copyright © 2012. Morogoro Yetu - All Rights Reserved
Template Modify by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa