Home » » Wanakijiji wa Pwaga walilia wanaotelekezwa na mimba

Wanakijiji wa Pwaga walilia wanaotelekezwa na mimba

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 

 Wananchi wa Kijiji cha Pwaga katika Wilaya ya Mpwapwa wamewataka wajumbe wa Bunge Maalumu la Katiba kuweka vipengele kuhusu haki za wasichana wanaopewa mimba na kutelekezwa.
Wakichangia maoni yao katika mdahalo juu ya utawala bora juzi, wananchi hao walisema vitu vingi vimeachwa ndani ya Rasimu ya Katiba.
Mdahalo huo uliitishwa na Muungano wa Asasi za Kiraia wilayani Mpwapwa, (Ngomnet) kwa ufadhili wa The Foundation for Civil Society.
“Mambo mengine ni ya msingi kabisa. Tusipoangalia yanaweza kutuyumbisha. Mimi nakerwa sana na tabia ya vijana wa kiume wanaowapa mimba watoto wetu wa kike na baadaye kuwatelekeza.Hili likiwekwa kisheria hata ndani ya Katiba litasaidia sana,” alisema Edward Chiwanga.
Chiwanga alisema tabia hiyo imeanza kuota mizizi katika maeneo mengi na kwamba imekuwa ikisababisha wasichana kukatisha masomo. Alisema hali hiyo inatokea wakati wanaume hao hawachukuliwi hatua.
Akitoa mada katika mdahalo huo, Edward Mbogo aliwataka wajumbe wa Bunge Maalumu la Katiba kufanya uamuzi wa busara ili kujenga nchi.
Alisema wajumbe hao wanapaswa kuhakikisha kuwa wanaondoka Dodoma wakiwa wamoja na nchi kubaki kuwa moja.
Mbogo alisema kinachosubiriwa na Watanzania si malumbano kuhusu posho au namna ya kupiga kura ya siri au wazi, bali katiba yenye matumaini kwa wote.
Kuhusu utawala bora, alisema bado watu wengi hawajui jinsi ya kupata haki zao za msingi na kwamba wamekuwa wakiziomba badala ya kuzidai.
Alisema wakati wote haki zinakwenda na wajibu hivyo kama wananchi wametimiza wajibu wao hawatakiwi kuomba haki.
Wakati huo huo, vikundi vya wanawake katika Manispaa ya Morogoro, vimemwomba mbunge wa Jimbo la Morogoro mjini, Abdulaziz Abood kuhakikisha anatetea kupatikana kwa haki na masilahi ya wanawake kwa namna yalivyopendekezwa na makundi ya wanawake nchini ili yaweze kuingizwa katika Katiba Mpya.
Wanawake hao walisema hayo mjini Morogoro wakati wakipokea msaada wa vifaa mbalimbali pamoja na hundi kutoka kwa mbunge huyo ambayo ilikuwa ni ahadi yake kwa vikundi hivyo baada ya kufanya ziara. Alishauri mapendekezo ya wanawake ni vizuri yakaingizwa katika Katiba mpya kwani wao ndiyo wamekuwa na jukumu kubwa la kuelimisha jamii na familia kwa ujumla.
Akizungumza kwa niaba ya wanawake wenzake, Mwenyekiti wa Kikundi cha Slab Vicoba cha Polisi, Ukende Ugula alisema suala la kuhakikisha wanawake wanapata nafasi za viongozi nusu kwa nusu na wanaume lizingatiwe ili kuweka usawa katika maamuzi ya ngazi zote.
Ugula alisema kuwa bado wanawake wamekuwa wakidharauliwa na kundi kubwa la wanaume hasa wale waishio vijijini na kukabiliwa na changamoto za kutengwa bila sababu za msingi mpaka kusababisha vifo visivyotarajiwa katika familia.
Akikabidhi msaada huo mbunge huyo aliwataka wanawake hao kuhakikisha wanatumia kwa manufaa ya jamii wanayoiongoza ikiwa ni pamoja na kuinuka kiuchumi ili kuondokana na utegemezi
Chanzo;Mwananchi

0 comments:

 
Supported by : Tone Media
Copyright © 2012. Morogoro Yetu - All Rights Reserved
Template Modify by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa