Home » » Wakulima walia na DC Mvomero

Wakulima walia na DC Mvomero

MKUU wa Wilaya (DC) ya Mvomero, Anthony Mtaka, mmiliki wa Kiwanda cha Sukari Mtibwa na Mkuu wa Polisi wa Wilaya (OCD), wanadaiwa kuukacha mkutano wa wakulima wa miwa wa nje wa  Mtibwa ulioitishwa kujadili hatima ya deni la sh bilioni 1.9 linalodaiwa na wakulima hao kiwandani hapo msimu uliopita.
Wakizungumza kwa nyakati tofauti mwishoni mwa wiki kwenye mkutano huo ulioitishwa na vyama vya siasa kikiwemo Chama Cha Mapinduzi (CCM), Chama cha Wananchi (CUF) na Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) wilayani humo, wakulima hao walisema walisikitishwa na kitendo cha mkuu huyo wa wilaya kutotokea kwenye mkutano huo.
“Sisi ni wanyonge hatuwezi kuwafanya kitu…unadhani hata wakija hapa watasema nini kama wamechukua miwa yetu tangu Agosti 2013 na hawajatulipa? Dawa ni kuvamia kiwanda tugawane kilichopo,” alisema Julius Shekilima wa Kidudwe.
Walisema mkuu huyo wa wilaya amekuwa hana msaada kwao, kwani  licha ya kumfikishia tatizo la kutolipwa fedha zao kwa zaidi ya mara tano aliahidi kufuatilia bila mafanikio.
“Sasa watoto hawasomi, hatuna fedha za kujikimu, tumekopa kila kona hadi hatutoki majumbani, tukiuuliza uongozi wa kiwanda hauna jibu zaidi ya kutukejeli na kutudharau eti madai yetu hayakitishi kiwanda,” alisema Husina Saleh wa Madizini.
Waandaaji wa mkutano huo akiwemo Diwani wa Mtibwa, Lucas Mwakambaya, walifafanua kuwa uwepo wa mkutano huo haukuwa siri kwani wakulima, mmiliki wa kiwanda na mkuu huyo wa wilaya walikuwa na taarifa isipokuwa walipuuza.
“Unajua hizi kazi za kuwatumikia wananchi zinahitaji wenye nia thabiti ya kuwatumikia wananchi. Mfano hili suala ukilianagalia kwa mfumo wa serikali tuliyonayo ni hadi yatokee maafa utaona msururu wa viongozi hata wasiotarajiwa kufika huku daima,” alifafanua Mwaka Mbaya.
Alieleza inashangaza wanachi waliosota mwaka mzima hawalipwi madai yao halali na hakuna hata jibu kwa umma juu ya ucheleweshwaji.
Kutokana na hali hiyo, wakulima hao walikubaliana kesho kuingia kiwandani hapo kwa nguvu kushinikiza walipwe fedha zao vinginevyo aende Waziri Mkuu, Mizengo Pinda,  kutatua mgogoro huo.
“Ndugu zetu si wakulima wanaodai kiwanda hiki, wastaafu wa mwaka jana walilipwa kiwango cha makadirio ya shilingi 700,000 kati ya shilingi milioni tano hadi 10, eti fedha nyingine watalipwa kwa awamu,” aliongeza.
Mtaka alipotafutwa  ili kutoa ufafanuzi juu ya kutotokea kwenye mkutano huo, alijibu kwa ukali na kwa kifupi, akimtaka mwandishi kuandika ajuavyo.
“Sina sababu yoyote ya kutohudhuria mkutano ule…wewe andika ujuavyo bwana…” alisema Mtaka kisha kukata simu.
Kiwanda cha Sukari Mtibwa wilayani Mvomero kimekuwa na mgogoro na wakulima na wafanyakazi wake kwa muda mrefu sasa. 
Chanzo;Mwananchi

0 comments:

 
Supported by : Tone Media
Copyright © 2012. Morogoro Yetu - All Rights Reserved
Template Modify by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa