Home » » Sekondari ya William Lukuvi wanafunzi walala darasani

Sekondari ya William Lukuvi wanafunzi walala darasani

Wiki iliyopita nilikwenda Morogoro ambako pamoja na mambo mengine nilikuwa na kipindi kwenye televisheni moja mkoani humo, kilicholenga kutoa ushauri kwa jamii kuhusu namna ya kupambana na changamoto za maisha. Baadaye nilikutana na watu waliokuja kwenye hoteli niliyokuwepo kwa lengo la kubadilishana mawazo zaidi kuhusiana na yale ambayo niliyaeleza kwenye televisheni. Mmoja wa watu alikuwa ni Erick Mtengele, kijana wa Kimasai ambaye amekuwa akihangaika huku na kule kutafuta namna ya kuwasaidia wafugaji nchini.
 “Mimi ni kati ya Wamasai wachache nchini walio na elimu ya chuo kikuu, nimehitimu elimu ya maendeleo ya jamii katika Chuo Kikuu cha Tumaini mwaka 2010, kwa bahati mbaya hadi leo sina ajira,” anasema Mtengele ambaye ni mzaliwa wa Kijiji cha Luganga, Kata ya Ilala Mpya, mkoani Iringa.
Tulizungumza mengi, yakiwemo matatizo ya sekta ya elimu nchini na harakati zake za kuwasaidia wanafunzi wa Shule ya Sekondari ya William Lukuvi wapate angalau bweni, akisema kuwa ameandika barua maeneo kadhaa kuomba shule hiyo ijengewe bweni bila mafanikio.
“Shule haina mabweni, wanafunzi wanalala kwenye madarasa,” anasema Mtengele.
Baada ya mazungumzo hayo nililazimika kufuatilia ili kujua ukweli, nilibaini kuwa ni ukweli thabiti kwamba wapo wanafunzi wanalala kwenye madarasa katika shule hiyo, sababu kubwa ni kwamba shule haina uwezo wa kifedha wa kujenga mabweni.
“Huogopi kufuatilia shule hii?” anaonya mwandishi mmoja wa habari anayefanyia kazi mkoani Iringa kwa maelezo kuwa kufuatilia shule hiyo kunaweza kuzusha kutokuelewana na baadhi ya watu ambao kwa namna moja ama nyingine wanahusika na shule hiyo.
Mwandishi huyo anaonya kuwa hofu ya kufanyiwa mabaya ndiyo sababu waandishi walio wengi wanaogopa kuandika ukweli kuhusiana na shule hiyo kwamba baadhi ya wanafunzi wanalala katika madarasa tofauti katika shule hiyo.
“Kuna  waandishi waliwahi kufuatilia suala hili na kuhoji kwa nini mabweni hayajengwi, matokeo yake siyo tu kwamba hawakupewa ushirikiano na wale ambao wanahusika kutolea maelezo jambo hilo, bali walionekana kama wanaingilia mambo yasiyowahusu, wengine hata wakajikuta katika hofu kuhusu maisha yao,” alionya mwandishi huyo.
Hata hivyo niliendelea kufuatilia kutokana na ukweli kwamba lengo la makala hii siyo kudhalilisha yeyote, bali kueleza ukweli ili kuangalia namna gani wanafunzi wanaweza kusaidiwa kwa kujengewa mabweni.
Kama yupo mwenye nguvu za kusumbua wale ambao wanaeleza ukweli kuhusiana na hali mbaya ya maisha ya wanafunzi kwa kukosa mabweni, nguvu hizo azielekeze kuhakikisha mabweni yanajengwa, tena ikiwezekana haraka.
Nguvu zake zitakuwa za maana zaidi ikiwa atafikiria namna ya kusaidia kupatikana kwa mabweni kuliko kukasirika kwa sababu ya kuandikwa ukweli kwamba Shule ya Sekondari William Lukuvi haina mabweni kiasi kwamba wanafunzi wanalazimika kulala darasani.
Katika kufuatilia ilibainika kuwa ni kweli kuna ugumu wa kupata ushirikiano, na pia hata baadhi ya waandishi wa habari wana hofu, kwa mfano kuna mwandishi alifanikiwa kupiga picha miezi kadhaa iliyopita wanafunzi wakiwa darasani wamelala, hakuweza kuzitumia, huku ulinzi ukiwekwa kuhakikisha hakuna mwandishi anayefanikiwa kufahamu hali hiyo ya watoto kulala darasani.

chanzo;mwananchi

0 comments:

 
Supported by : Tone Media
Copyright © 2012. Morogoro Yetu - All Rights Reserved
Template Modify by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa