Home » » Halmashauri Moro kujenga hospitali ya wilaya

Halmashauri Moro kujenga hospitali ya wilaya

HALMASHAURI ya Manispaa ya Morogoro inatarajia kupunguza msongamano wa wagonjwa katika Hospitali ya Rufaa mkoani hapa kwa kujenga hospitali ya wilaya ya manispaa hiyo katika eneo la Kikundi, nje kidogo ya mji kwa gharama ya sh bilioni mbili.
Meya wa Manispaa ya Morogoro, Amir Nondo, alibainisha hayo mjini hapa jana alipozungumza na waandishi wa habari na kusema kuwa tayari mkataba wa ujenzi huo umesainiwa na Kampuni ya Mzinga Co-operation kwa ajili ya kuanza ujenzi.
Nondo alisema kampuni hiyo itaanza na ujenzi wa nyumba ya mapokezi ambayo itakamilika katika kipindi cha siku tisini na kwa gharama ya sh milioni 548 na baadaye kuendelea na majengo mengine.
Alisema ujenzi wa hospitali hiyo utasaidia kupunguza msongamano kwenye hospitali ya rufaa ya mkoa ambapo mgonjwa atatibiwa kwenye zahanati za kata na ikishindikana atapelekwa kwenye hospitali hiyo.
“Lengo letu mgonjwa ikishindikana kutibiwa kwenye zahanati zetu ambazo tumejenga kila kata, atapewa rufaa kwenda hospitali ya wilaya na hapo kama bado atapelekwa hospitali ya rufaa ya mkoa, si mtu anapata kihoma kidogo anakimbilia hospitali ya mkoa, tunataka kupunguza mrundikano wa wagonjwa,” alisema.
Pia alibainisha hospitali hiyo inatarajia kujengwa katika kipindi cha mwaka mmoja, na kwamba hadi kufikia mwaka 2014 mwishoni wanatarajia huduma iwe imeanza kutolewa.
Chanzo: Tanzania Daima

0 comments:

 
Supported by : Tone Media
Copyright © 2012. Morogoro Yetu - All Rights Reserved
Template Modify by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa