SEKTA ndogo ya tumbaku nchini inakabiliwa na
changamoto kadhaa na endapo zitapatiwa ufumbuzi wa kudumu, zao hilo litawanufaisha
maradufu Watanzania.
Mkurugenzi wa mambo ya sheria wa kampuni za
Tanzania Leaf Tobacco (TLTC) pamoja na Tanzania Tobacco Processors Limited
(TTPL), Richard Sinamtwa, aliorodhesha changamoto kadhaa zinazoikabili sekta
ndogo ya tumbaku wakati akiwasilisha taarifa yake kwa Mkuu wa Mkoa wa Morogoro,
Joel Bendera, alipotembelea TTPL.
Alisema sekta hiyo inaandamwa na changamoto nyingi
ikiwemo ya tozo, ushuru wa mazao unaolipwa kwa halmashauri za wilaya wakati wa
kuvuna tumbaku, ushuru wa huduma ambao unalipwa mahali ambako kiwanda cha
kuchakata tumbaku kimejengwa pamoja na kodi inayotokana na faida.
“Hili ni zao lile lile linalotoka shambani hadi
kiwandani, lakini linakatwa kodi zaidi ya moja kinyume cha sheria za kodi,”
alisema.
Sinamtwa alisema changamoto nyingine inayoikabili
sekta ndogo ya tumbaku ni zao hilo kushindwa kupigiwa debe, ili liingie kwenye
soko la Marekani kupitia mpango wa ukuzaji fursa za kiuchumi Afrika (Agoa),
hasa kwa vile nchi hiyo hutoza ushuru wa idadi maalumu iliyowekwa (TRQ) kwa baadhi
ya mazao ya kilimo kama vile cocoa, karanga, sukari na tumbaku.
“Utaratibu wa TRQ unaruhusu idadi maalumu ya bidhaa
kuingizwa katika soko la Marekani bila kulipiwa ushuru au kwa kiwango maalumu
kwa kipindi fulani cha muda, lakini pale kiwango cha bidhaa kinapozidi idadi
inayotakiwa, basi kinakatwa kodi zaidi,” alisema Sinamtwa.
Alimtaka mkuu wa mkoa kufikisha kilio hicho kwa
Wizara ya Viwanda na Biashara, ili kuliwezesha zao la tumbaku kuingia kwenye
soko la Agoa.
Alisema matatizo mengine yanayokumba uzalishaji wa
zao la tumbaku ni uwezo mdogo wa bandari ya Dar es Salaam, ambao unasababisha
baadhi ya bidhaa zinazoonekana zinaweza kuharibika haraka pamoja na mafuta
kupewa kipaumbele zaidi dhidi ya makontena ya tumbaku na bidhaa nyingine.
“Hali hii inasababisha ucheleweshaji usio wa lazima
katika kusafirisha tumbaku, hivyo kuleta athari katika taratibu nzima za
kusafirisha tumbaku nje,” aliongeza.
Sinamtwa alisema matatizo mengine yanayoikabili
TPPL, ni umeme usioaminika katika uzalishaji, na hivyo kukifanya kiwanda muda
mwingi kutumia jenereta.
Kuhusu mafanikio, Sinamtwa alisema ni ongezeko la
thamani ya mtaji, ikiwa ni pamoja na mali za kampuni, ambazo zimepanda kutoka
dola milioni 15.6 za Marekani mwaka 1997 wakati kampuni iliponunua kiwanda
kutoka kwa kampuni iliyokufa ya Tanzania Tobacco Authority hadi kufikia dola
milioni 57 mwaka 2012, ongezeko ambalo ni takriban asilimia 276.
Pia kodi inayokatwa baada ya faida ilipanda kutoka
sh bilioni 1.7 mwaka 2008 hadi sh bilioni 2.2 mwaka jana huku gawio wanalopata
wadau likipanda kutoka sh milioni 104 mwaka 2008 hadi sh milioni 165 mwaka
jana.
Mkuu wa Mkoa, Bendera, aliahidi kufanyia kazi
changamoto zinazokabili uzalishaji wa tumbaku nchini kwa kuwasiliana na mamlaka
zinazohusika.
Akitoa neno la shukrani, mkurugenzi mkuu wa
makampuni hayo mawili, Paul Crossan, alimshukuru Bendera kwa kuwatembelea,
akisema ni ziara aliyoifanya kwa wakati muafaka na ina umuhimu mkubwa kwa
maendeleo ya sekta ndogo ya tumbaku.
Chanzo: Tanzania Daima
0 comments:
Post a Comment