Home » » 80% CCM watimuliwa kwa ubadhirifu

80% CCM watimuliwa kwa ubadhirifu

ZAIDI ya asilimia 80 ya watumishi wa Jumuiya ya Wazazi ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) wamefukuzwa kazi kwa tuhuma za kusababisha madeni na miradi ikiwamo shule kufilisika.
Mjumbe wa Baraza Kuu la jumuiya hiyo taifa, William Malecela, alisema hayo wakati wa mkutano wa ndani wa Halmashauri Kuu ya CCM Manispaa ya Morogoro na kudai kuwa watumishi wengine  zaidi watafukuzwa ili kuiweka jumuiya hiyo katika hali nzuri na kurudi katika heshima yake.
“Watumishi wengi wameiingiza jumuiya katika madeni makubwa  na kuiacha haina fedha na hata miradi yetu mbalimbali ya maendeleo kama shule inakufa sasa, tunataka turudi katika msitari,” alisema Malecela.
Alisema uongozi wa sasa umekusudia kuifufua upya jumuiya hiyo, na wale wanaoona hawawezi kwenda na kasi iliyopo, ni vema wakajiondoa wenyewe na kupisha wengine.
“Tuliingia madarakani akaunti ya jumuiya ikiwa haina senti, lakini sasa akaunti ina fedha, hata mikutano ya baraza tunaiendesha kwa kujilipa wenyewe, hatutegemei kuomba.
“Mwakani kama mambo yatakwenda vizuri, tumekusudia kila mkoa kuwa na gari, wilaya kuwa na pikipiki na kata baiskeli, ingawa wapo wasiotutakia mema kutokana na kuwanyima ugali kutokana na namna walivyokuwa wameigeuza jumuiya hii,” alisema Malecela.
Akiwa Morogoro Vijijini, Mwenyekiti wa Jumuiya ya Wazazi, Abdallah Bulembo, aliwaasa madiwani kutogeuka miungu watu katika maeneo yao, na kuwataka kuthamini chama kilichowatuma katika nafasi hizo, badala ya kujiona wao ni watumishi wa serikali.
Chanzo: Tanzania Daima

0 comments:

 
Supported by : Tone Media
Copyright © 2012. Morogoro Yetu - All Rights Reserved
Template Modify by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa