Home » » Jaji Mwambegele kuchunguza migogoro ya ardhi Morogoro

Jaji Mwambegele kuchunguza migogoro ya ardhi Morogoro

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 

Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, William Lukuvi
WIZARA ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi kwa mara ya kwanza katika historia imelazimika kumteua Jaji kwa ajili ya kufanya uchunguzi wa migogoro ya ardhi iliyoshindikana kupatiwa suluhu kwa njia ya usuluhishi katika vijiji saba mkoani Morogoro.
Akizungumza Dar es Salaam jana, Waziri wa wizara hiyo, William Lukuvi alisema amemteua rasmi Jaji wa Mahakama Kuu, Kitengo cha Biashara, Jacob Mwambegele kwa mujibu wa Sheria ya Ardhi kufanya uchunguzi wa migogoro hiyo kwa muda wa siku 60 akiwa na timu ya wataalamu wanane.
Alisema hatua hiyo ya kumteua Jaji kufanya uchunguzi kwa mujibu wa sheria imefikiwa baada ya wizara hiyo kuchukua hatua zote za kutafuta suluhu katika vijiji hivyo, vikiwemo viwili ambavyo migogoro yake imekithiri ambavyo ni Kambala kilichopo wilayani Mvomero na Mabwegere kilichopo wilayani Kilosa.
“Hii ni hatua yetu ya mwisho kama wizara katika kutafuta suluhu kwenye vijiji hivi, hasa hivi vya Kambala na Mabwegere ambavyo vilianzishwa rasmi mwaka 1989 vina migogoro mingi iliyosababisha maafa kwa binadamu, wanyama na mimea. Hivyo tunahitaji tu kufuata sasa hatua za kisheria,” alisisitiza Lukuvi.
Alisema kabla ya uteuzi wa Jaji Mwambegele, wizara hiyo ilishamteua msuluhishi Stephen Mashishanga ambaye jitihada zake za kusuluhisha migogoro hiyo zilishindikana na hata taarifa yake ya usuluhishi katika vijiji hivyo ilikataliwa na wananchi.
Lukuvi alisema kwa mujibu wa Sheria ya Ardhi endapo hatua zote za kutafuta suluhu katika migogoro ya ardhi zitashindikana, hatua inayofuata ni kumchagua mtu atakayefanya uchunguzi wa migogoro hiyo mwenye uzoefu kisheria ili hatua za kisheria zichukuliwe.
Chanzo Na Habari Leo

0 comments:

 
Supported by : Tone Media
Copyright © 2012. Morogoro Yetu - All Rights Reserved
Template Modify by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa