Home » » SEKTA BINAFSI YALILIA MITAJI YA MASHARTI NAFUU ILI KUJIIMARISHA

SEKTA BINAFSI YALILIA MITAJI YA MASHARTI NAFUU ILI KUJIIMARISHA

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 

Wafanyabiashara wadogo na wa kati wamekuwa katika wakati mgumu wa kupanua biashara zao kutokana na taasisi za fedha kutoa mitaji ya muda mfupi kwa ajili ya kuendesha biashara badala ya kutoa mitaji ya muda mrefu yenye masharti nafuu.
Utaratibu huo wa taasisi za fedha umesababisha biashara kukua polepole na kukwamisha fursa nyingi za kibiashara, licha ya wafanyabiashara wadogo na wa kati kutoa mchango mkubwa katika uchumi wa taifa.
Kutokana na kuwapo kwa changamoto hiyo, mwaka huu waandaji wa bajeti wameshauriwa kuifanyia kazi Sera ya Uchumi na Uwezeshaji ya Taifa ya mwaka 2004 kwa lengo la kuiwezesha sekta binafsi kujiendesha katika mazingira mazuri.
Lakini siyo hayo tu, bali licha ya kuwapo kwa mifuko ya fedha za uwezeshaji kwa mfano, mfuko wa uwezeshaji wa mwananchi na mfuko wa uwezeshaji wa uchumi na mpango wa ajira (J.K. Fund), upatikanaji wa mitaji umekuwa ni tatizo kwa wafanyabiashara kutokana na kutokuwapo kwa mazingira rafiki kwenye taasisi za fedha.
Kwa mtazamo wa jicho la pili, Tanzania imejitahidi kuanzisha taasisi za kukopesha wafanyabiashara kwa mfano, Benki ya Maendeleo Tanzania (TIB), lakini imeshindwa kuzipatia fedha za kutosha kwa ajili ya kutoa mikopo ya muda mrefu kwa wafanyabiashara.
Kwa mujibu wa utafiti kuhusu wafanyabiashara wadogo na wa kati, uliofanywa na Atsede Woldie, John Isaac Mwita na Joyce Saidimu, taasisi za fedha zimeshindwa kuwawezesha wafanyabiashara hao kutokana kukosa maarifa ya kuendesha miradi ya kibenki na kuwapo kwa gharama kubwa katika utoaji wa huduma za kifedha.
Kutokana na mazingira hayo, sekta binafsi imeishauri Serikali kuweka mazingira mazuri ya kupatikana kwa mitaji ya kutosha katika bajeti ijayo.
Mbali na hoja hizo, wafanyabishara hao kwa nyakati tofauti wanasema kuwa mazingira magumu ya upatikanaji wa mikopo kutoka taasisi za fedha, ni kikwazo cha kutokua kwa biashara zao.
Mhadhiri wa uchumi wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Profesa Humphrey Moshi anasema serikali inapaswa kuzishawishi benki ili zitoe huduma maalumu za kifedha kwa wafanyabiashara.
Profesa Moshi anasema benki hizo zinapaswa kutoa mikopo ya muda mrefu yenye masharti nafuu kwa wafanyabiashara kwa lengo la kukuza biashara zao.
“Kwa mfano, benki zote za India, zina madirisha maalumu kwa ajili ya kusaidia shughuli za kilimo na madirisha mengine maalumu yanayotoa huduma za kifedha kwa wafanyabiashara wadogo na wa kati. Mkakati huo unapaswa ufanyike hapa kwetu. Naamini kama serikali itafanya hivyo uchumi wa taifa utakua vizuri.
“Sekta isiyo rasmi nchini ina wafanyabiashara wadogo milioni 3 ambao wanachangia asilimia 48 ya uzalishaji wa ndani na kutengeneza ajira nchini kwa asilimia 26.
“Wafanyabishara wa wadogo na kati ni kundi muhimu katika ukuaji wa uchumi katika mataifa duniani pia wanatengeneza ajira mbalimbali. Serikali inapaswa kuwasaidia wafanyabiashara ili wapate mikopo yenye masharti nafuu na kuinua biashara zao,” anasema Profesa Moshi.
Profesa Moshi anaishauri Benki Kuu ya Tanzania (BoT) kuzifuatilia taasisi za fedha ili zipunguze riba katika mikopo inayotoa kwa wafanyabiashara.
“Kumekuwapo kwa ongezeko kubwa la taasisi za fedha kama vile, Ushirika wa Kuweka na Kukopa (Saccos) na Vikoba ambazo hazifuatiliwe BoT. Taasisi hizi zinatoa mikopo kwa riba kubwa na wakati mwingine wanachangia kufa kwa biashara kutokana na wakopaji kushindwa kurejesha mikopo,” anaeleza Profesa huyo.
Mkurugenzi mtendaji wa mfuko wa sekta binafsi, Godfrey Simbeye anasema katika bajeti ijayo, Serikali inapaswa kutenga fedha kwa ajili ya kutoa mafunzo kwa wajasiriamali kama inavyofanya katika sekta nyingine nchini.
“Elimu kwa wajasiriamali ni muhimu kwa kuwa wengi wanashindwa kufanya biashara kitaalamu,” anaeleza Simbeye.
Simbeye anasema Serikali inapaswa kuboresha Wizara ya Viwanda na Biashara na kuongeza fedha zaidi TIB kwa lengo la kuiwezesha kutoa mikopo ya muda mrefu kwa wafanyabiashara.
Kwa mujibu wa Simbeye, mitaji imekuwa ni tatizo kwa wafanyabiashara kwa kuwa wengi wao wameshindwa kufanya biashara na wenzao wa nje ya nchi.
“Kuwekeza katika miradi mikubwa, unapaswa kuwa na fedha nyingi na hii inawezekana, endapo taasisi za fedha zitakuwa zikitoa fedha za kutosha, lakini hilo Tanzania halifanyiki.
“Serikali ina wajibu wa kutuwezesha kupitia benki yake ya TIB, ili iwe rahisi kwa sekta binafsi kukopa fedha nyingi kwa ajili ya miradi mbalimbali.
“Katika mwaka huu wa fedha, sijui Serikali imetenga shilingi ngapi katika Benki ya TIB, lakini naamini kwamba kiasi cha fedha kilichotengwa hakitatosha kwa ajili ya miradi ya maendeleo,” anabainisha Simbeye.
Katika hatua nyingine, Simbeye anasema katika mpango wa maendeleo wa mwaka 2011/12 hadi 2015/16, sekta binafsi inatakiwa kuchangia Dola 6 bilioni za Kimarekani kila mwaka ikiwa ni kutekeleza mpango huo.
Chanzo:Mwananchi

0 comments:

 
Supported by : Tone Media
Copyright © 2012. Morogoro Yetu - All Rights Reserved
Template Modify by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa