Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399.
Wakazi wa Jiji la Dar es Salaam wakichimba udongo chini ya Daraja la
Mto Msimbazi lililopo Tabata Matumbi jana kutafuta miili ya ndugu zao
waliozolewa na mafuriko kutokana na mvua zinazoendelea kunyesha katika
maeneo mbalimbali ya jiji.
Watoto watano wamekufa maji katika maeneo mbalimbali mkoani
Morogoro na mwingine Dar es Salaam jana baada ya kutumbukia kwenye mito
na mashimo yaliyofurika maji ya mvua kubwa zinazoendelea kunyesha
nchini.
Vifo hivyo vinafanya idadi ya watu walipoteza
maisha tangu mvua hizo kubwa zilipoanza Aprili 10, mwaka huu kufikia
takriban 16 na kusababisha uharibifu mkubwa wa miundombinu ya barabara,
makazi ya watu na mazao.
Mkuu wa Wilaya ya Kilosa, Elias Tarimo alisema
jana kwamba mwanafunzi wa kidato cha kwanza katika Shule ya Sekondari
Kilosa, anahofiwa kufa maji baada ya kuzama katika Mto Ludewa
alipojaribu kuvuka akitokea shuleni.
Tarimo alisema hadi kufikia jana asubuhi, mwili wa mwanafunzi huyo ambaye jina lake halijafahamika, ulikuwa bado haujapatikana.
Habari kutoka Kilombero zinasema watoto wawili wa
familia moja katika Kitongoji cha Godauni, Kijiji cha Mkangawalo, Tarafa
ya Mngeta, wamekufa maji baada ya kutumbukia kwenye shimo.
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Morogoro, Faustine
Shilogile aliwataja watoto hao kuwa ni Festo Andrew (3) na Chrisantus
Mnanagali (11) na kwamba walitumbukia shimoni baada ya kuteleza
walipokuwa wakicheza.
Shilogile alisema katika tukio jingine, watoto
wengine wawili wa familia moja, nao walikufa maji baada ya kuzama
walipokuwa wakivuka Mto Morogoro katika eneo la Mlimani.
Hata hivyo, alisema wazazi na ndugu wa watoto hao
waligoma kutoa taarifa polisi na badala yake walichukua miili ya
marehemu iliyokuwa imehifadhiwa katika Hospitali ya Rufaa Morogoro.
Taarifa zilizotolewa na Wakuu wa Wilaya za
Kilombero, Kilosa, Ulanga na Mvomero, mvua hizo zimeathiri kwa kiasi
kikubwa mashamba, miundombinu ya barabara, majengo ya umma na makazi ya
wananchi.
Mkuu wa Wilaya ya Kilombero, Hassan Masala alisema
Barabara za Mlimba- Ifakara na Chita-Mbingu, zimefungwa na huduma za
usafiri zimesitishwa kutokana na uharibifu huo.
Alisema tayari ameshatoa taarifa kwa Wakala wa
Barabara Tanzania (Tanroads), ili kufanya tathmini ya uharibifu wa
barabara hizo na kufanya matengenezo ya haraka ili kurudisha huduma za
usafiri.
Mkuu wa Wilaya ya Ulanga, Francis Miti alisema
mvua hizo zimesababisha uharibifu mkubwa katika Tarafa ya Malinyi ambako
baadhi ya barabara hazipitiki.
Alisema nyumba na mashamba mengi vimeharibiwa na mvua hizo na tayari amewatuma maofisa wake kufanya tathimini ya uharibifu huo.
Mkuu wa Wilaya ya Mvomero, Anthony Mtaka alisema
Barabara ya Mgeta-Nyandira imesombwa na maji hivyo kukwamisha huduma za
mawasiliano na uchukuzi. Barabara hiyo kwa sasa imefungwa kwa muda hadi
hapo itakapofanyiwa matengenezo.
Katika Manispaa ya Morogoro, barabara
zilizoharibiwa na mvua ni Barabara Kuu ya Morogoro - Dodoma eneo la
Kihonda Mbuyuni jirani na Mto Ngerengere ambako imeanza kutitia.
Tanroads imeifunga upande mmoja ili kuepusha maafa hali ambayo
imesababisha foleni na usumbufu kwa abiria na watumiaji wengine.
Mmoja afariki Dar
Taarifa za Polisi Mkoa wa Ilala zimesema mtu mmoja
aliyetambulika kwa jina moja Mkojani (30) alifariki dunia juzi saa 11
jioni maeneo ya Segerea kwa Bibi alipokuwa akivuka maji.
Akizungumza jana, Kamanda wa Polisi Mkoa wa Ilala,
Marietha Minangi alisema mtu huyo alikuwa akiendesha bodaboda na
alikufa baada ya kupita kwenye maji hayo na kuingia katika dimbwi
lililokuwa na nyaya za umeme na kusababisha kifo chake.
Alisema watu walioshuhudia tukio hilo walisema mtu
huyo alikaidi wito wa kutopita hapo kutokana na kuanguka kwa nyaya
hizo. Katika tukio jingine alisema mkondo wa maji unaounganisha Chanika
na Nyeburu umefurika na kusababisha eneo la Barabara ya Chanika
kukatika.
Kwa upande wake, Kamanda wa Mkoa wa Temeke,
Engelbert Kiondo alisema Daraja la Mto Kizinga lililopo Kongowe ambalo
linaunganisha Kigamboni na Mbagala limepata ufa na halifai kutumika.
“Hali ni mbaya sana ninavyokueleza nipo hapa na
nimeshindwa kupitisha gari langu. Tunawaomba wananchi wasipitishe magari
yao eneo hili kwa kuwa muda wowote linaweza likakatika,” alisema
Kiondo.
Arusha yachukua tahadhari
Mkoa wa Arusha umeanza kuchukua tahadhari ya
kukabiliana na madhara ya mafuriko kwa kuviweka tayari vikosi na
kukusanya vifaa vya uokoaji.
Pamoja na vikosi na vifaa vya uokoaji, uongozi wa
mkoa pia umeanza kukusanya bidhaa mbalimbali kama magodoro, mashuka,
mablanketi na vyakula kwa ajili ya waathirika iwapo eneo lolote ndani ya
mkoa litakumbwa na mafuriko.
Mkuu wa Mkoa wa Arusha, Magessa Mulongo alisema licha ya tukio la kukatika kwa daraja linalounganisha Wilaya za Monduli na Karatu eneo la Mto wa Mbu, hakuna jingine la mafuriko lililotokea mkoani mwaka huu hadi kufikia jana mchana.
Chanzo;mwananchi
Mkuu wa Mkoa wa Arusha, Magessa Mulongo alisema licha ya tukio la kukatika kwa daraja linalounganisha Wilaya za Monduli na Karatu eneo la Mto wa Mbu, hakuna jingine la mafuriko lililotokea mkoani mwaka huu hadi kufikia jana mchana.
Chanzo;mwananchi
0 comments:
Post a Comment