Home » » 'NASHUKURU KWA KUPATA MAPACHA WATATU LAKINI...'

'NASHUKURU KWA KUPATA MAPACHA WATATU LAKINI...'

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399.
Mapacha watatu
Kujifungua salama ndio matarajio ya wazazi wengi na furaha yao huionekana mara tu baada ya kujifungua. Mzazi hufarijika aonapo mtoto aliye mikononi mwake yu salama.
Pamoja na ukweli huu, wako wanaoliona suala la kupata mtoto kama changamoto kubwa inayohitaji msaada madhubuti katika kukabiliana nalo.
Wakati mwingine wazazi wanaokuwa katika hali hii hulazimika kuingia hapa na pale ili kupata riziki itakayompa uhai kiumbe aliyemfikia.
Hiki ndicho kilichotokea kwa Rehema Kachala (37), mkazi wa Kimamba wilayani Kilosa, ambaye hivi karibuni alijaliwa kujifungua mapacha watatu ambao ni Ibrahim, Ikram na Islam.
“Nimejifunga watoto hawa watatu kwa njia ya upasuaji. Huu ni uzazi wangu wanne na umenifanya niwe na watoto sita,” anasema.
Rehama alijifungua watoto hao katika Hospitali ya Taifa ya Muhimbili mapema mwezi huu, lakini je ilikuwaje akajifungulia Muhimbili na sio Kilosa anakoishi?
“Mimi ni mkazi wa Kimamba, wilayani Kilosa mkoani Morogoro. Nikiwa mama wa nyumbani, kazi yangu ni mkulima kama ilivyo kwa wanawake wengi vijijini,” anasema.
Anasema alipata ujauzito mwishoni mwa mwaka jana na kwa bahati nzuri alihudhuria mapema kliniki, jambo lililosaidia kugunduliwa kwa watoto hao watatu katika ujauzito wake.
“Tangu kupata habari hizo nilikosa raha kwani pamoja na ukweli nilikuwa nikihitaji kupata mtoto. Nilikuwa nahofia hatma yangu na watoto wangu,” anasema.
Mawazo yote yalikuwa ni jinsi gani angeweza kujifungua salama na kuwanusuru watoto wake wote watatu.
Kinachoniumiza
“Kilichokuwa kikiniumiza ni huu umasikini kwani najua kwa uwezo wa familia yangu tusingeweza kupata pesa kwa ajili ya kujihudumia, hasa katika kipindi hiki kigumu,” Anasema.
Wakati akiwaza na kuwazua wakati uliyoyoyoma na hata kufikia kipindi cha kukaribia kujifungua.
“Baadhi ya ndugu walichangishana na kupata pesa na kunisafirisha kuja kujifungua jijini Dar es Salaam ambako nilikuwa na imani kuwa ningeweza kujifungua chini ya uangalizi wa kutosha wa wataalamu wa afya,” anasema.
Jijini Dar es Salaam
Alifika jijini Dar es Salaam na kufikia kwa kaka yake anayeishi eneo la Kimanga Darajani, Tabata.
“Nilikaa kwa muda wa wiki moja ndipo Julai 7 mwaka huu hali yangu ikazidi kuwa mbaya kuwa tangu nipate ujauzito nilikuwa nikisumbuliwa na shinikizo la juu la damu. Siku hiyo nilizidiwa nikapelekwa Zahanati ya Tabata, ambako baadaye nilipelekwa Amana,” anasema.
Kutokana na kuwa na hali mbaya, madaktari wa Hospitali ya Amana walimpa rufaa na kwenda Hospitali ya Taifa Muhimbili.
“Nikiwa huko nilipata matibabu ya shinikizo la damu, huku nikisububiria kujifungua. Lakini kabla ya kujifungua hali ilikuwa mbaya zaidi na hivyo madaktari wakalazimika kunifanyia upasuaji ili kunusuru maisha yangu na watoto,” anafafanua.
Kweli upasuaji ulifanikiwa na akajaaliwa kupata watoto watatu wa kiume wakiwa na afya ya kuridhisha.
Pamoja na kujifungua salama, bado changamoto kubwa ni katika ulezi wa watoto hao. Kwani kwa sasa watoto hao wanahitaji chakula cha ziada, kutokana na ukweli kuwa hamudu kuwashibisha wote kwa wakati mmoja.
“ Naomba Serikali inisaidie katika malezi ya watoto hawa, kwani kwa umri waliokuwa nao maziwa ndio chakula pekee wanachoweza kula, lakini pia ningeomba mnisaidie nguo kwa ajili yao,” anasema.
Anasema kwa kuwa sasa ni kipindi cha baridi, hofu kubwa aliyonayo ni watoto wake hao kupata magonjwa yanayosababishwa na baridi kama vile homa ya mapafu na hata kukohoa.
“Ikiwa nitapata maziwa na hata mavazi yao, ni wazi kuwa nitapata ahuweni katika ulezi wao. Kwa sasa nimekuwa nikiishiwa nguvu kutokana na kunyonywa kwa muda mrefu, ninakosa hata muda wa kupumzika kutokana na kunyonywa mchana na usiku kucha,” anabainisha.
Anasema hata wakinyonya, wanaonekana hawashibi na hivyo kuwa changamoto kubwa kwake kuwarodhisha
Chanzo:Mwananchi

0 comments:

 
Supported by : Tone Media
Copyright © 2012. Morogoro Yetu - All Rights Reserved
Template Modify by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa