Home » » TEA KUFADHILI UJENZI WA NYUMBA ZA WALIMU KATIKA MAENEO YASIO RAHISI KUFIKIKA

TEA KUFADHILI UJENZI WA NYUMBA ZA WALIMU KATIKA MAENEO YASIO RAHISI KUFIKIKA

Mkurugenzi  Mkuu wa Mamlaka ya Elimu Tanzania Joel Laurent (wa kwanza kushoto) akijadiliana suala  na viongozi wa Halmashauri ya Kilosa, Mamlaka ya Elimu  Tanzania inatarajia kutekeleza na kufadhili mradi wa kujenga nyumba za walimu kupitia Watumishi Housing Ltd katika Ujenzi katika maeneo yasio rahisi kufikika, katika shule ya Sekondari Uleling'ombe iliyopo Wilaya ya Kilosa.
 Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Elimu Tanzania,Joel Laurent akiongea na viongozi wa Halmashauri ya Wilaya ya Kilosa, kamati ya shule ya Uleling'ombe,uongozi wa kijiji cha Uleling'ombe wakijadilana utekelezaji wa Mradi wa kujenga nyumba za walimu katika maeneo yasio rahisi kufikika, katika shule ya Sekondari Uleling'ombe iliyopo Wilaya ya Kilosa.
 Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Elimu Tanzania,Joel Laurent akioneshwa eneo lililotengwa kwa ajili ya kujenga nyumba za walimu katika shule ya Sekondari Uleling'ombe mradi unaotekeleza na kufadhili na Mamlaka ya Elimu Tanzania ikiwatumia Watumishi Housing Ltd katika Ujenzi katika maeneo yasio rahisi kufikika.
Picha ya pamoja.

Na Mwandishi Wetu

MKURUGENZI Mkuu wa Mamlaka ya Elimu Tanzania (TEA), Joel Laurent amesisitiza kuwa taasisi yake itaendelea kutafuta rasilimali ili kuhakikisha kuwa wanafunzi wanosoma katika maeneo ambayo ni magumu kufikika wanajengewa miundombuni ili kupata elimu bora.

Mkurugeni Mkuu huyo alisema hayo wilayani Kilosa wakati akikagua eneo la ujenzi wa nyumba ya walimu wa shule ya sekondari ya Uleling’ombe utakaogharimu zaidi ya 148m/- ambayo walimu sita watakaa katika nyumba hiyo.

Alisema mamlaka hiyo imetiliana saini mkataba na Watumishi Housing wa ujenzi wa nyumba za walimu 40 nchi nzima katika maeneo ambayo ni magumu kufikika ili kuhakikisha kuwa walimu wapya wanaopangiwa katika maeneo hayo ambao wengi wamekuwa wakikimbia kufundisha wanapata sehemu nzuri za kuishi.

Aliongeza kuwa katika mwaka huu wa fedha mamlaka yake imetenga bajeti ya kujenga nyumba 30 mwaka huu ambapo ujenzi wa kila nyumba ni miezi mitatu.
“Nyumba hii itakapokuwa tayari na tunategemea ikamilike ifikapo Desemba mwaka huu, itakuwa na uwezo wa kuwaweka walimu sita kuishi katika nyumba hiyo ila tunazitaka halmashauri kuangalia uwezekano wa kuwawekea samani za ndani” alisema.

 
Na pia alisisitiza juu ya umuhimu wa ushiriki wa wananchi na halmashauri hizo katika kuhakikisha kuwa ujenzi wa nyumba hizo unazingatia ujenzi ili ziweze kutumika kwa muda mrefu na hivyo kuwanufaisha wanafunzi wengi zaidi.

TEA ilibuni mradi huo baada ya kugundua kuwa kuna uhitaji maalum wa makazi ya walimu katika mazingira ambayo ni vigumu kufikika ambapo wengi ambao wamekuwa wakipangiwa kufundisha hutafuta uhamisho na hivyo wanafunzi wa maeneo hayo ufaulu wao umekuwa mdogo kutokana na kukosa walimu.

“Walimu wanaokusudiwa kuishi katika nyumnba hizi ni wale wanaoanza kazi ndiyo maana ni chumba na sebule kwa kila mwalimu kwani tunaamini baada ya muda watakuwa wameishazoea na kuweza kujipatia makazi uraiani pale watakapokuwa tayari kuanza familia” Alisema Bw Laurent.

Aliongeza kuwa mamlaka hiyo inajadiliana na wadau mbali mbali ili kuona kama wataweza kuwezesha upatikanaji wa internet na ving’amuzi katika sebule ya pamoja ya nyumba hizo ili wale watakaopangiwa maeneo hayo wasijione kuwa wamepangiwa katika mazingira ambayo si rafiki au wameonewa.

Akizungumza katika ukaguzi huo, Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Kilosa, Bw Rwegerela Katabaro alisema kuwa wako tayari kushirikiana na TEA japo rasilimali fedha imekuwa ni changamoto kubwa.

Aliomba kuwa katika miradi mingine halmashauri zipewe taarifa za awali ili ziweke kutenga fungu katika bajeti zaona hivyo kuchangia katika juhudi za maendeleo.
Alimhakikishia Mkurugenzi Mkuu huyo juu ya ushiriki wa halmashauri kusimamia kwa karibu ujenzi wa nyumba hiyo ili kupata nyumba ambayo inalingana na thamani ya fedha zilizotengwa.

Aidha ili kuondoa mgongano alishauri TEA itoe muongozo ili kila taasisi ijue jukumu lake katika kuhakikisha kuwa ujenzi wa nyumba hiyo unakuwa bora na kwa viwango walivyokubaliana.

Naye Mkuu wa Shule ya Sekondari Uleling’ombe, Magashi Shimba alishukuru kwa kupatiwa mradi huo kwani walimu wengi wanaopangiwa huko huwa hawarudi kutokana na mazingira hasa upatikanaji wa makazi.

0 comments:

 
Supported by : Tone Media
Copyright © 2012. Morogoro Yetu - All Rights Reserved
Template Modify by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa